23.3 C
Dar es Salaam
Saturday, April 20, 2024

Contact us: [email protected]

Lembeli ataka Lowassa asafishwe

Na Khamis Mkotya, Dodoma
MBUNGE wa Kahama Mjini, James Lembeli (CCM), ameaungana na Mbunge wa Kigoma Mjini, Peter Serukamba, baada ya kuzungumzia ripoti ya Katibu Mkuu Kiongozi, Ombeni Sefue iliyowasafisha baadhi ya watendaji serikalini waliohusika katika kashfa ya Escrow na Operesheni Tokomeza.
Akichangia bungeni jana, Lembeli alisema wakati Serikali imewasafisha baadhi ya watendaji, haoni jitihada kama hizo za kumsafisha Mbunge wa Monduli, Edward Lowassa aliyejiuzulu uwaziri mkuu kutokana na kashfa ya Richmond.
Lembeli alikuwa akichangia Hoja ya Bajeti ya Ofisi ya Waziri Mkuu, Mizengo Pinda aliyoiwasilisha bungeni juzi akiomba Sh trilioni 5 kwa mwaka wa fedha wa 2015/2016.
Lembeli ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Maliasili, Utalii na Mazingira, alishangazwa na taarifa hiyo iliyowasafisha baadhi ya watu waliohusishwa katika kashfa hiyo na kuwaacha wengine, jambo ambalo alisema halitoi taswira ya usawa.
Katika mchango wake, Lembeli alisema haoni mantiki kwa Serikali kumsafisha Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini, Eliackim Maswi na Waziri Profesa Sospeter Muhongo na kuwaacha wengine.
Katika mchango wake juzi Serukamba alijikita zaidi katika kashfa ya Escrow wakati Lembeli alijikita katika kashfa ya Operesheni Tokomeza.
Mapema mwezi huu, Katibu Mkuu Kiongozi, Ombeni Sefue, alisema uchunguzi dhidi ya Profesa Muhongo na Maswi, umebaini kuwa viongozi hao hawakukiuka maadili yoyote katika suala hilo.
Mbali na viongozi hao, uchunguzi mwingine wa malalamiko ya utekelezaji wa Operesheni Tokomeza uliosababisha waliokuwa mawaziri watatu kujiuzulu, pia umebaini mawaziri hao hawakujihusisha moja kwa moja na upungufu wa operesheni hiyo.
Viongozi hao ni aliyekuwa Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Dk. Emmanuel Nchimbi na aliyekuwa Waziri wa Maendeleo ya Mifugo na Uvuvi, Dk. David Mathayo David.
Wengine ni aliyekuwa Waziri wa Maliasili na Utalii, Balozi Khamis Kagasheki na aliyekuwa Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Shamsi Vuai Nahodha.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles