27.9 C
Dar es Salaam
Thursday, March 28, 2024

Contact us: [email protected]

Lema apandishwa kizimbani Singida, asomewa mashtaka 15

Nathaniel Limu -Singida

MBUNGE wa Arusha Mjini, Godbless Lema, amepandishwa kizimbani katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Singida jana, akituhumiwa kwa makosa 15 yakiwamo ya mtandaoni.

Mwendesha mashtaka wa Serikali, Monica Mbogo, alidai mbele ya Hakimu Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Singida, Consolate Singano, kuwa Februari 29 mwaka huu huko Manyoni, mshtakiwa akiwa kwenye mazishi ya kiongozi wa Chadema, alipotosha jamii kwa kutoa taarifa za uongo.

Monica alidai katika kosa la kwanza, Lema alisababisha taharuki kwa jamii kwa kitendo chake cha kusambaza mitandaoni taarifa za upotoshaji.

Alidai katika makosa mengine 14, Lema kwa kutumia kompyuta yake alisambaza taarifa za watu 14 kwamba wamechinjwa jambo ambalo si kweli.

Monica alitaja watu ambao Lema alidai kuwa wamechinjwa na makazi yao kwenye mabano ni Sechelela Moses, (Manyoni mjini), Abdallah Lyanga (Itigi), Rajabu Abas (Itigi) na Martiner Mtekwa (Manyoni mjini).

Wengine ni Hamad Hussein (Aghodi), Emmanuel Messo (Maweni), Mika Saimoni (Mkoko), Nyembelele Njezo (Mitundu), John Lugion (Makale), Michael Charles (Mwamagembe) na Issa Abdala (Sajalanda), Jumanne Ndelemo (Sajilila), Heri Mambo (Solya) na Alex Jonas (Manyoni mjini).

Mshtakiwa ambaye anawakilishwa na wanasheria wa kujitegemea; Mwiru Amani na Hemed Nkulungu, alikana makosa yote hayo.

Hakimu Singano alitoa masharti ya dhamana kuwa mshtakiwa anapaswa kuwa na wadhamini wawili wanaoaminika na kutoa ahadi ya dhamana ya shilingi milioni tano kila mmoja.

Lema alitimiza sharti hilo la dhamana, na yupo nje hadi Aprili 15 kesi yake itakapotajwa tena.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles