27.2 C
Dar es Salaam
Friday, April 19, 2024

Contact us: [email protected]

SABABU YA VYUO VYA KITAFITI KUTAMBA ORODHA YA VYUO VIKUU

Na MWANDISHI WETU,

KATIKA orodha nyingi za vyuo vikuu bora duniani, nafasi 10 au 20 za juu mara nyingi hung’ang’aniwa na taasisi maarufu za kisayansi za Marekani na Uingereza.

Hizo ni pamoja na Teknolojia ya Massachusetts (MIT), Taasisi ya Teknolojia California (Caltech), Imperial College London cha Uingereza, Chuo Kikuu cha Cambridge, pia cha Uingereza.

Nyingine ni Chuo Kikuu cha Harvard, Marekani, ambacho ni taasisi ya elimu ya juu tajiri kabisa duniani, Chuo Kikuu cha College London na Oxford vya Uingereza na kadhalika.

Hata hivyo ukiondoa Marekani na Uingereza kuna Taasisi ya Teknolojia ya Shirikisho Uswisi maarufu kama ETH Zurich.

Asia pia inajivunia Chuo Kikuu cha Taifa Singapore (NUS) na Chuo Kikuu cha Kiteknolojia Nanyang (NTU), Chuo Kikuu cha Peking cha China.

Kwanini vyuo vya kitafiti zaidi ndivyo huibuka katika orodha ya ubora?

Pamoja na kwamba baadhi ya viongozi wa vyuo vikuu duniani huhoji vigezo vinavyotumika kuorodhesha ubora wa vyuo hivyo, bado wanatambua umuhimu wake.

Mkuu wa Udahili katika Chuo Kikuu cha Oxford, Mike Nicholson anasema: “Ni sawa kusema kwamba itakuwa upuuzi kwa chuo kikuu kupuuza namna orodha ya ubora wa vyuo inavyopangwa.”

Uorodheshaji ubora wa vyuo umekuwa sehemu isiyokwepeka ya sifa na taswira ya vyuo vikuu, ikivisaidia kunasa wanafunzi, wafanyakazi na uwekezaji wa tafiti.

Lakini kile kinachoonekana zaidi kushangaza ni kuwa taratibu hizi hazina muda mrefu, yaani ni za miaka ya karibuni katika muktadha wa elimu ya juu.

Kuna ligi mbalimbali kama Times Higher Education, ligi ya QS na ile orodha ya awali ya kimataifa, Academic Ranking of World Universities.

Lakini namna gani chuo kikuu kinaweza kushika nafasi ya juu katika orodha hizo? Na kwanini kundi dogo la taasisi za elimu ya juu linaonekana kung’ang’ania katika nafasi ya juu miaka yote?

Kipengele kikubwa kabisa katika orodha ya QS kwa mfano ni sifa ya kitaaluma. Sifa hiyo hukokotolewa kwa kutafiti wasomi zaidi ya 60,000 duniani kuhusu maoni yao juu ya sifa nzuri za taasisi nyingine zaidi ya zile zao wenyewe.

Mkurugenzi Mtendaji wa QS, Ben Sowter anasema kuwa hilo linamaanisha kuwa vyuo vikuu vilivyojijengea umaarufu kwa muda mrefu vina uwezekano wa kufanya vyema zaidi.

Kipengele kingine cha pili kikubwa – ‘mtajo kwa kila kitivo’ –kuangalia nguvu ya tafiti ya vyuo vikuu, ambayo hukokotolewa kwa kuzingatia idadi ya kazi za kitafiti za chuo kikuu husika zilizotajwa au kunukuliwa na watafiti wengine.

Uwiano wa wafanyakazi wa taaluma na wanafunzi unawakilisha kipengele kingine kikubwa cha tatu cha namna orodha ya ubora inavyoamuliwa.

Elementi hizo tatu, sifa njema, kutajwa mara nyingi kitafiti na uwiano wa wafanya kazi, huchukua nne ya tano ya uorodheshaji huo.

Na pia kuna alama nyingine zinazohusu hadhi ya ukimataifa linapokuja suala la wafanyakazi na wanafunzi wa chuo husika.

Sifa ya kitaaluma ya Chuo Kikuu cha Harvard ni kipengele kikubwa kinachoibeba katika orodha hiyo kwa miaka mingi.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles