24.2 C
Dar es Salaam
Friday, April 19, 2024

Contact us: [email protected]

Kuzaliwa kwa Baghdadi hadi kuwa kiongozi wa IS

MWANDISHI WETU

ABU Bakr al-Baghdadi, ni kiongozi wa kundi la Kijihad la Islamic State (IS) na mtu ambaye alikuwa akisakwa mno duniani. Kwa mujibu wa Rais wa Marekani, Donald Trump, Baghdadi alijiua kufuatia uvamizi wa Marekani uliotekelezwa na kikosi maalum cha wanajeshi Kaskazini Magharibi mwa Syria.

Marekani ilikuwa imetangaza kutoa kitita cha Dola milioni 25 kwa yeyote atakayewezesha kupatikana kwa taarifa kuhusu mahali alipo Abu bakr al Baghdadi.

‘Kalifa Ibrahim’ kama ambavyo alipenda kujiita, alikuwa akisakwa na Marekani na washirika wake tangu kuanzishwa kwa kundi la IS miaka mitano iliyopita.

IS lilidhibiti kilomita za mraba 88,000  za eneo kutoka magharibi mwa Syria hadi mashiriki mwa Iraq, na likaweka utawala wake wa ukatili kwa zaidi ya watu milioni nane, huku likijipatia mabilioni ya madola kutokana na mapato ya mafuta, wizi na utekaji nyara.

Lakini licha ya kuangamizwa kwa utawala wao na kiongozi wake, IS inasalia kuwa kundi kali la kivita na kikosi chenye nidhamu ya hali ya juu ambapo hakuna uhakika wa kuangamizwa kwake.

Wasifu wake

Baghdadi alizaliwa mwaka 1971 katika Mji wa kati wa Iraq kwa unaoitwa Samarra. Jina lake la kuzaliwa ni Ibrahim Awwad Ibrahim al-Badri na Familia yake ni ya Kiarabu kutoka madhehebu ya Sunni, inayodaiwa kutoka katika kabila la Mtume Muhammad la Quraysh – kitu kinachoaminika kuwa sifa ya kuwa Kalifa.

Akiwa kijana, ndugu zake walimpa jina la utani ‘Muumin’ kwa sababu muda mwingi aliutumia akiwa ndani ya msikiti akisoma Qur-an na kwamba mara kwa mara aliwashutumu walioshindwa kufuata sheria ya Kiislamu au sharia.

Baada ya kumaliza shule mapema miaka ya 1990; alielekea katika Mji Mkuu wa Baghdad. Alijipatia shahada na shahada ya uzamifu katika mafunzo ya Kiislamu kabla ya kusomea stashahada katika Chuo Kikuu cha Kiislamu cha Baghdad. Kulingana na wasifu wake uliochapishwa na wafuasi wake.

Akiwa mwanafunzi, aliishi karibu na Msikiti wa Kisunni katika Mji wa Kasakazini Magharibi wa Baghdad, Wilaya ya Tobchi.

Anasemakena kuwa ni mtu mtulivu aliyewekuwa msiri wa mambo yake isipokuwa wakati alipokuwa akijifunza kusoma Qur-an na kuichezea soka klabu ya msikiti huo.

Baghdadi anaaminika kukumbatia Jihad na salafi wakati huo.

Aunda kundi la wapiganaji

Kufuatia mashambulizi ya Marekani yaliyompindua Rais Saddam Hussein mwaka 2003, Baghdadi aliripotiwa kuanzisha kundi la wapiganaji wa Kiislamu lililoitwa Jamaat Jaysh Al al- Sunnah wa-al-Jamaah ambalo lilishambulia vikosi vya Marekani na washirika wao.

Ndani ya kundi hilo, alikuwa kiongozi wa kamati ya sharia. Mapema mwaka 2004, Baghdadi alikamatwa na wanajeshi wa Marekani katika Mji wa Faluja, Magharibi mwa Baghdad, na kupelekwa katika kambi moja ya Bucca Kusini.

Kambi ya Bucca ilikuwa kile ilichoelezewa kuwa chuo cha viongozi wa siku zijazo, huku wafungwa wakipewa itikadi kali na kupata mawasiliano muhimu.

Askari wa jeshi la Marekani

Baghdadi aliripotiwa kuongoza ibada, alitoa hotuba na kufundisha madarasa ya kidini akiwa kizuizini na mara nyengine alitakiwa kuingilia kati ili kutatu mizozo na utawala wa Marekani katika kambi hiyo.

Hakuonekana kama mwenye tishio kubwa na Marekani na alitolewa baada ya miezi 10.

Mmoja wa maafisa wa Pentagon aliliambia gazeti la The New York Times kuwa Baghdad alikuwa mhalifu wa barabarani alipokamatwa mwaka 2004/2014. ”Ni vigumu kufikiria kwamba angekuwa kiongozi wa IS.”

Kuunda al-Qaeda nchini Iraq

Baada ya kuondoka kambi ya Bucca, Baghdad anaaminika kuwasiliana na uongozi mpya wa al-Qaeda nchini Iraq.

Chini ya uongozi wa Abu Musab al – Zarqawi, Al – Qaeda lilibadilika na kuwa kundi kubwa katika uvamizi huo wa Iraq na kupata sifa kwa ukatili wake, ikiwamo kuchinja watu vichwa.

Mapema mwaka 2006. Al Qaeda iliunda baraza la Jihadi kwa jina Mujahideen Shura, ambalo Baghdad liliahidi kutii na kujiunga nalo.

Baadaye mwaka huo, kufuatia kifo cha Zarqawi aliyefariki kutokana mashambulizi ya angani ya wanajeshi wa Marekani, shirika hilo lilibadili jina lake hadi kundi la Islamic State nchini Iraq.

Baghdadi alisimamia kamati ya ISI na kujiunga na baraza hilo la Shura.

Wakati kiongozi wa ISI Abu Umar al- Baghdadi alifariki kutokana na mashambulizi ya Marekani ya mwaka 2010 pamoja na naibu wake Abu Ayyub al- Masri, Abu bakr al- Baghdadi alitajwa kuwa mrithi wake.

Alirithi shirika ambalo makamanda wa Marekani waliamini linakaribia kushindwa. Lakini kupitia usaidizi wa wanajeshi kadhaa wa Saddam na maafisa wa Kijasusi, miongoni mwao wafungwa wenza wa kambi ya Bucca alianza kuijenga upya ISI.

Lilikotokea jina Kalipha Ibrahim

Mapema 2013, lilikuwa likitekeleza mashambulio kadhaa kwa mwezi nchini Iraq.

Pia lilishiriki katika pingamizi dhidi ya utawala wa Rais Assad, akituma wanajeshi wa Syria kurudi Iraq baada ya kuunda kundi la al- Nusra Front kama mshirika wa al- Qaeda nchini humo.

Wakiwa hapo, waliweza kupata silaha kwa urahisi.

14

Mwezi Aprili, Baghdadi alitangaza kuunganishwa kwa vikosi vyake nchini Iraq na Syria na uundaji wa kundi la Islamic State nchini Iraq na lile la Isil.

Viongozi wa al – Nusra na al-Qaeda walikataa hatua hiyo, lakini wapiganaji walio watiifu kwa Baghdad walijiondoa katika al-Nusra na kulisaidia Isis kusalia Syria.

Mwishoni mwa mwaka 2013, Isis ilirudi Iraq na kusababisha hali ya sintofahamu kati ya serikali ya madhehebu ya Kishia na walio wachache wa madhehebu ya Sunni ambao ni Waarabu.

Wakisaidiwa na makabila yao na waliokuwa wandani wa rais Saddam Hussein, Isis iliiteka Faluja.

Juni 2014, wanajeshi kadhaa wa Isis waliteka Mji wa Mosul, wakilifurusha jeshi la Iraq na baadaye kuelekea kusini mwa Baghdad, wakiwaua wapinzani wao na kutishia kuyaangamiza makabila mengi ya walio wachache.

Mwisho wa mwezi, baada ya kuteka makumi ya maeneo ya miji ya Iraq, Isis ilitangaza uongozi wa Kiislamu – taifa linaloongozwa kwa mujibu wa sharia za Kiislamu na kulitaja kuwa taifa la Kiislamu Islamic State.

Ulimtangaza Baghdadi kuwa Kalipha Ibrahim na kutaka utiifu kutoka kwa Waislamu wote duniani.

Siku tano baadaye, kanda ya video ilitolewa ikimuonyesha Baghdadi akitoa hotuba katika Msikiti Mkuu wa Mosul wa al- Nuri, – ikiwa mara yake ya kwanza kuonekana katika kamera.

Wataalam walisema kwamba hotuba za Baghdadi zilifanana na zile zilizotolewa na makalifa wa karne ya kwanza wa Kiislamu.

Aliwaomba Waislamu duniani kuhamia katika eneo la Islamic State ili kusaidia Waislamu kupigana dhidi ya wasioamini. Makumi ya maelfu ya wageni walielekea katika eneo hilo ili kuitikia wito huo.

Mwezi mmoja baadaye, wapiganaji wa IS waliingia katika maeneo yanayodhibitiwa na Wakurdi walio wachache nchini Iraq na kuwaua mbali na kuwateka maelfu ya watu wa kabila hilo wanaotoka katika dini ya Yazidi.

Ukatili huo dhidi ya Yazidi, ambao wachunguzi wa Umoja wa mataifa walisema unashirikisha uhalifu wa kimbari, ulisababisha kuundwa kwa muungano unaoongozwa na Marekani ambao ulianza kampeni ya angani dhidi ya wapiganaji wa kijihadi nchini Iraq.

Muungano huo ulianza mashambulizi ya angani nchini Syria Septemba, baada ya IS kuwachinja mateka kadhaa wa Magharibi.

IS ilijibu mashambulizi ya moja kwa moja dhidi ya muungao huo unaoongozwa na Marekani, wakiutaja kama vita dhidi ya adui wa Waislamu vilivyotabiriwa na hadithi za mitume.

Katika maeneo yaliopo chini ya udhibiti wake, IS iliweka sheria ya Kiislamu iliokuwa ikiwanyanyasa wakaazi.

Wanawake waliotuhumiwa kushiriki ngono nje ya ndoa walipigwa mawe hadi kufa, mikono ya wezi ilikatwa huku wale waliotuhumiwa kupinga uongozi wa IS walikatwa vichwa.

Rubani mmoja wa Jordan ambaye ndege yake ilianguka karibu na Raqqa Luteni Moaz al-Kasasbeh alichomwa moto hadi kufa.

Kundi hilo lilizua hisia kali duniani kwa kuharibu majengo ya kuonyesha vitu vya kale kutoka mji wa jangwani wa Palmyra , hadi katika mji wa Assyrian wa Nimrud nchini Iraq na kuiba vitu hivyo vya kale katika majumba hayo hayo ya kumbukumbu.

Kitengo cha utamaduni cha Umoja wa Mataifa – Unesco, kilishutumu uharibifu huo kama uhalifu wa kivita.

Mashambulio katika mataifa mengine pia yalianza kudaiwa kutekelezwa na IS ama watu binafsi walioshinikizwa na kundi hilo.

Mshambulio kama hayo, ikiwamo kuangushwa kwa ndege ya Urusi katika anga ya Misri eneo la rasi ya Sinai, Oktoba 2015, mashambulio ya Paris na mauaji ya kujitoa muhanga ya Sri lanka Aprili 2019 – yamesababisha mauaji ya maelfu ya watu tangu 2014.

Baghdadi yeye binafsi alishutumiwa kwa kumbaka mara kwa mara mfanyakazi wa shirika moja la kibinafsi kutoka Marekani ambaye alikuwa akizuiliwa, Kayla Mueller, kabla ya kumuua.

Maafisa wanasema kwamba waligundua ukatili huo kutoka kwa wasichana wawili wa Yazidi.

Kushindwa kwa IS

Wakati muungano unaoongozwa na Marekani ulipoingilia kati, IS ilianza kuondolewa polepole katika eneo ililokuwa ikilidhibiti.

Vita hivyo vilisababisha mauaji ya maelfu ya watu katika mataifa hayo mawili, kuwaacha mamilioni bila makao na kuharibu eneo zima.

Nchini Iraq, vikosi vya kijimbo pamoja na wapiganaji wa Kikurdi wa Peshmerga walioungwa mkono na Muungano huo wa vikosi vya Marekani vilitawaliwa na wanaanga kutoka Iran.

Nchini Syria, muungano huo unaoongozwa na Marekani uliunga mkono muungano mwengine wa wapiganaji wa Kikurdi kutoka Syria na wapiganaji wa Arabuni, Jeshi la Syria pamoja na waasi wa Syria katika jangwa la kusini.

Wanajeshi walio watiifu kwa Rais Assad wakati huohuo waliwakabili wapiganaji wa IS kupitia usaidizi wa mashambulizi ya Urusi na wapiganaji wa Iran.

Katika vita hivyo, swali la iwapo Baghdadi alikuwa hai au amekufa lilikuwa likiwachanganya wengi.

Juni 2017, wakati vikosi vya Iraq vikiwakabili wapiganaji wa IS mjini Mosul, maafisa wa Urusi walisema kwamba kulikuwa na uwezo mkubwa kwamba Baghdadi aliuawa katika shambulio la angani la Urusi kandokando mwa mji wa kaskazini wa Syria wa Raqqa ambao ndio uliokuwa mji mkuu wa IS.

Lakini, kufikia Septemba IS ilitoa ujumbe wake wa sauti kutoka kwa Baghdadi ulioshirikisha simu iliyokuwa ikiwaambia wafuasi wa kundi hilo kukabiliana na wapinzani wa dini ya Kiislamu.

17

Tangazo hilo halikutosha kuwazuia wanajeshi wa SDF kuteka mji wa Raqqa mwezi uliofuata na kuwasukuma wafuasi wake katika jangwa.

Kufikia Agosti 2018; Baghdadi alitoa ujumbe mwingine kwa njia ya sauti.

Aliwataka wafuasi wake nchini Syria kuwa na subira wakati walipokuwa wakishindwa katika eneo la vita.

Mwezi uliofuata, wapiganaji wa SDF walianzisha kampeni yao ya mwisho ya kuwafurusha wapiganaji wa IS kutoka kwa mashariki mwa Syria wakilenga ardhi inayopitia ziwa Euphrates karibu na mji wa Hajin ambapo makumi ya maelfu ya wapiganaji wa IS na familia zao walikusanyika baada ya kutoroka Mosul na Raqqa.

Hakukuwa na ishara kwamba Baghdadi alikuwa kati yao, lakini habari ambazo hazikuthibitishwa zilijitokeza baadaye kwamba alilazimika kutorokea katika jangwa la magharibi la Iraq baada ya kundi moja la IS kujaribu kum’ngoa madarakani.

Machi mwaka huu, eneo la mwisho lililokuwa likidhibitiwa na IS nchini Syria, karibu na Kijiji cha Baghuz lilitekwa na wanajeshi wa SDF, na hivyo kumaliza rasmi utawala wa Kalipha wa Baghdadi.

Rais wa Marekani Donald Trump aliusifu uhuru huo wa Syria huku akisema: “Tutaendelea kuwa waangalifu dhidi ya IS.”

Vita kumaliza nguvu za adui

IS ilidaiwa kusalia kuwamiliki maelfu ya wapiganaji wake katika eneo hilo, wengi wao wakitekeleza operesheni zao katika seli.

Nchini Iraq, walikuwa wakitekeleza mashambulio kwa lengo la kukandamiza utawala wa serikali, kutengeneza mazingira yasio kuwa na sheria kufuatwa, kuhujumu maridhiano na juhudi za ujenzi.

Aprili mwaka huu, Baghdadi alionekana katika kanda ya video kwa mara ya kwanza katika kipindi cha miaka mitano.

Lakini badala ya kuzungumzia kutoka kwa mimbari ya msikiti mjini Mosul, wakati huu alikuwa ameketi katika sakafu ya chumba kimoja akiwa na bunduki kando yake.

Alikiri kuhusu kushindwa kwa kundi lake na kusema kwamba IS ilikuwa ikipigana vita vya kupunguza nguvu za adui, akiwataka wafuasi wake kutekeleza mashambulio yatakayowafurusha wapinzani wao, kupitia wanadamu, kijeshi, kiuchumi na rasilimali za kimkakati.

Haikubainika ni lini au wapi kanda hiyo ya video ilirekodiwa, lakini Baghdadi alionekana kuwa buheri wa afya.

Alionekana akiwa ameketi na takriban watu watatu ambao nyuso zao zilikuwa zimefichwa na kupitia faili za wanachama wa IS katika matawi kadhaa kote duniani.

Pia aliwataka wafuasi kuwaaachilia huru maelfu ya washukiwa wa IS na makumi ya maelfu ya wanawake na watoto wanaohusishwa na IS ambao walikuwa wakizuiliwa katika jela za SDF na kambi za Syria kufuatia kukombolewa kwa Baghuz.

Mwezi uliofuata, shambulio la Uturuki dhidi ya SDF kaskazini mashariki mwa Syria na hatua ya Rais Trump kuondoa vikosi vya Marekani kutoka katika eneo hilo badala yake ilizua hisia kwamba huenda IS ikatumia fursa iliyopo na kurudi.

Zaidi ya wafungwa 100 walitoroka wakati wa mashambulizi hayo huku seli zilizoangamizwa za IS zikitekeleza mashambulio kadhaa, lakini Rais Trump alikataa ukosoaji wa kuondoa vikosi vyake Marekani.

“Uturuki, Syria na wengine katika eneo hilo watalazimika kushirikiana ili kuhakikisha IS haichukui udhibiti wowote wa eneo hilo,” anasisitiza.

Rais Trump baadaye aliwaambia maripota kwamba, Baghdadi alijificha katika handaki moja na watoto watatu wakati wa uvamizi wa wanajeshi maalum wa Marekani na akalipua fulana yake ya ndani iliyofungwa vilipuzi wakati mbwa wa kijeshi wa Marekani walipotumwa kumsaka akijiua na watoto hao.

Hadi sasa hakuna tamko lolote kuhusu kifo cha Baghdadi kutoka kwa IS.

Makala hii imeandaliwa kwa msaada wa Shirika la Habari la BBC

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles