27.1 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

Kundi jipya limeibuka kuwatikisa wanasiasa, viongozi duniani

NA MARKUS MPANGALA

MABADILIKO makubwa duniani yametokea katika mfumo mzima wa siasa na demokrasia katika miaka ya hivi karibuni. Wakati dunia ikiwa imeonyesha kupoteza ladha ya wanasiasa na viongozi wenye sifa, wenye uwezo na karama ya uongozi ambao umetokana na mfumo wa kisiasa uliozoeleka, yameibuka makundi mengine ambayo yapo tofauti na mazoea yaliyokuwepo awali. 

Kuibuka kwa wachekeshaji,wanamuziki, waigizaji, wanasoka na wanamitindo wenye mvuto, ushawishi, nguvu, uwezo na kukubalika katika siasa na uongozi kunawatikisa wanasiasa waliopitia ukada wa vyama vyao vya siasa. 

Ulimwengu mpya wa teknolojia umechangia kwa kiasi kikubwa kuyaibua makundi hayo na kuongeza ushawishi, nguvu na kukubalika miongoni mwa wananchi, hivyo kuwalazimisha kujiingiza kwenye siasa na uongozi. 

Baadhi ya mataifa yakiwemo Marekani yamewahi kuongozwa na rais aliyekuwa mwigiziaji wa filamu huko Hollywood, Ronald Reagan. 

Ulimwengu wa tatu umeshuhudia kuibuka kwa kundi la wachekeshaji kuziteka siasa, kwakuwa wana wafuasi wengi kwenye mitandao ya kijamii hali ambayo inawavutia watu mbalimbali kuona busara, uwezo, nguvu na ushawishi ambao unafaa kuingizwa kwenye uongozi katika ngazi mbalimbali. 

Burudani na michezo imezidi kuwa gumzo duniani ambapo wanamichezo wamezidi kujizolea umaarufu na kuchaguliwa kuongoza mataifa yao.

Kwa muktadha huo ukiacha kundi la kwanza la burudani na michezo, lipo kundi jingine ambalo linawahusisha viongozi ambao kwa hakika hawakuwa sehemu au wapo nje ya mfumo wa kisiasa, lakini wakapata nguvu baada ya kuingia na baadaye kuchaguliwa na wananchi.

Hili ni kundi la kwanza la viongozi ambao wametoka nje ya mnyororo wa mfumo wa kisiasa. Hawa ni viongozi ambao wameingia kwenye siasa bila kubebwa na mfumo wa kisiasa wa nchi husika, badala yake wamejijenga wenyewe na kuibuka kuwa wanasiasa mahiri wanaopendwa na wapigakura sehemu mbalimbali duniani. 

Kundi hili linajumuisha wanasiasa watata ambao hulka na mienendo yao imekuwa ikitibua mambo na kuwatisha wanasiasa waliozoea kubebwa na mfumo wakati wote.

Katika kundi hili wamo viongozi kama Rais wa Marekani, Donald Trump, mwanasiasa Julius Malema (Kiongozi wa chama cha EFF Afrika Kusini), Marie Le Pen (Mwanasiasa mwenye kupendelea ubaguzi wa Ufaransa na kujitenga na Jumuiya ya Ulaya). Ingawa Marie Le Pen hakushinda urais wa Ufaransa, lakini ni mwanasiasa anayebeba alama zote za viongozi watata waliopata kutokea duniani.

Wachekeshaji,wanamuziki, wanamichezo

Kundi la pili wamo Waziri Mkuu wa Pakistan, Imran Khan ambaye alikuwa mchezaji wa mchezo wa Kriketi, Rais wa Liberia George Weah, ambaye amewahi kuwa mchezaji bora duniani, Afrika na mwanasoka aliyezichezea klabu maarufu duniani kama AS Monaco, AC Milan na Chelsea. Mwingine ni Jimmy Morale ambaye ni mchekeshaji yaani ‘komedi’ aliyeshinda uchaguzi wa Rais nchini Guatemala. Naye Ronald Reagan alikuwa mcheza sinema maarufu wa Hollywood ambaye aliukwaa Urais wa Marekani.

Nchini Tanzania wamo wanamichezo na wanamuziki kama vile Joseph Mbilinyi(Sugu), Joseph Haule (Profesa Jay), ambao wameshinda uchaguzi katika nafasi ya ubunge wa Mbeya Mjini na Mikumi kupitia Chama kikuu cha upinzani nchini – Chadema. Wanamitindo Jokate Mwegelo (Mkuu wa Wilaya ya Kisarawe na kada wa CCM), Msanii wa Bongo fleva Crayton Chipando (Baba Levo) Diwani wa Kata ya Mwanga Kaskazini, mkoani Kigoma kupitia chama cha ACT Wazalendo.

Hii ni tafsiri kuwa dunia inaelekea kubadilika kutoka kufuata siasa za mfumo rasmi na kuwaingiza watu ambao hawakuwahi kuwa sehemu ya mfumo huo, lakini wanabebwa na wapigakura wao ambao wameamua kuwachagua kutokana na ushawishi,uwezo na nguvu zao ambazo wamejijenga wenyewe bila kutegemea vyama vya siasa.

Nchini Uganda tunaye Mbunge wa Kyadondo Mashariki, Robert Ssentamu, maarufu Bob Wine ambaye ni mwanamuziki mashuhuri wa miondoko ya dancehall. Bob Wine kwa sasa amekuwa mwiba mchungu kwa utawala wa Rais wa Uganda Yoweri Museveni, akiwa anakubalika na kuwavutia maelfu ya vijana wanaomuunga mkono. Bob Wine alishinda kiti cha ubunge akiwa mgombea binafsi baada ya kutojiunga na chama chochote.

Katikati ya mjadala kuhusu nafasi ya wanamuziki, wanasoka,wanamitindo, wachekeshaji kwa ujumla wake, ndipo anaibuka Volodymyr Zelensky, nchini Ukraine. Huyu ni mchekeshaji ambaye amewavutia maelfu ya vijana na wapigakura nchini humo baada ya kujijenga mwenyewe badala ya kutegemea nguvu za chama. 

Kimsingi Zelensky ambaye atapambana katika duru ya pili ya uchaguzi na mpinzani wake Petro Poroshenko, anakuwa miongoni mwa waburudishaji wanaoteka siasa duniani.

Katika duru ya kwanza ya uchaguzi nchini humo imeonyesha mchekeshaji Zelensky kuwa mshindi wa duru ya kwanza ya uchaguzi, ukiwa ni ujumbe tosha kwa dunia juu ya mabadiliko ya kisiasa kutoka siasa za kihafidhina hadi siasa za kisasa ambapo watu waliopo nje ya vyama vya siasa wanaushawishi mkubwa kuliko waliomo ndani ya vyama vya siasa. 

Duru za kisiasa zinaonyesha Zelensky hana uzoefu wa kutosha kama walivyo waburudishaji na wanamichezo wengine lakini kukubalika kwake miongoni mwa wananchi wa Ukraine kunaelezewa kama pigo kwa wanasiasa wa vyama.

Zelensky ana umri wa miaka 41 ambaye amekuwa akiigiza kama rais katika filamu maarufu katika runinga nchini humo alishinda zaidi ya asilimia 30.5 ya kura duru la kwanza, dhidi ya 16.6 za Rais Petro Poroshenko.

Aidha, mchekeshaji huyo amemshinda mwanasiasa mwingine mkongwe ambaye ni Waziri Mkuu wa zamani Yulia Tymoshenko aliyeshika nafasi ya tatu katika uchaguzi huo akiwa na asilimia 13.2 ya kura katika uwanja mkubwa wa mapambano wa wagombea 39 katika uchaguzi huu wa urais nchini Ukraine.

Kwa upande mwingine wanamichezo hawa wamekuwa wakikosolewa kutokuwa na uzoefu kwenye siasa na sera. Watu wanaomkosoa mchekeshaji Zelenskiy ni sawa na ambavyo hapa nchini wasanii wanavyokosolewa kutokana na wapinzani wao kutumia uzoefu mdogo kwenye siasa na sera kama kigezo cha kuwapinga. Lakini idadi kubwa ya wapigakura imethibitisha kuwa na imani nao, hali ambayo inabomoa mfumo wa kisiasa. 

Mwanzoni huwa tunaambiwa kuwa wanamichezo hao ni chaguo baya kwa taifa, lakini kadiri muda unavyozidi kusonga mbele tunagundua kuwa wale wanasiasa waliojikita kwenye mfumo wao hawawataki hawa wanasiasa wa kisasa ambao hawajapitia vyama vyao. 

Ni tatizo la wahafidhina, si hawana wanamuziki, wanamitindo, wacheza filamu na wanasoka. Dunia inazidi kubadilika, tuendako wanasiasa kutoka kwenye michezo na burudani watazidi kutam

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles