Asha Bani-Dar es salaam
Mbunge wa Ubungo Saed Kubenea, amelaani vikali watu wanaoshiriki kuvujisha, kurekodi na kusambaza kwa watu taarifa za mitandao ya simu ambapo amesema watu hao wanatakiwa kuchukuliwa hatua.
Ametoa kauli hiyo leo Jumatatu Julai 22, jijini Dar es Salaam, alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari, ambapo ameitaka Mamlaka ya Mawasiliano nchini (TCRA), kujitathimini na kuacha kuruhusu kufanya udukuzi wa sauti za watu kama lilivyo sakata la viongozi mbalimbali wa Chama cha Mapinduzi (CCM).
Amesema ni jambo la ajabu pale viongozi wanapofanya mazungumzo yao na kisha kuwekwa wazi kwa mfululizo wa muendelezo wa mazungumzo hayo.
“Hii ni hatari sana kama viongozi wanafanywa hivi kwa mambo ya faragha kutolewa si hata baadaye watu wanaweza kuvunja ndoa za watu, kama Mbunge wa Mtama, Nape Nnauye amezungumza na hawara kwa mfano ikatoka nje si jambo la hatari hili, kuna vitu ambavyo vinatakiwa kuwa na usiri kwa maana kama hawa ni viongozi tu je wananchi wa kawaida inakuaje,” amesema.