29.2 C
Dar es Salaam
Thursday, April 18, 2024

Contact us: [email protected]

KOMBE LA ASFC: YANGA MAJARIBUNI TENA

MOHAMED KASSARA-DAR ES SALAAM

TIMU ya Yanga imepangwa kucheza na Alliance FC katika mchezo wa robo fainali ya Kombe la Shirikisho (ASFC), utakaochezwa Uwanja wa Kirumba, Mwanza.

Mchezo huo unatarajiwa kuchezwa mwishoni mwa mwezi huu.

Droo hiyo imezikutanisha kwa mara nyingine Yanga na Alliance, baada ya timu hizo kuumana siku chache zilizopita katika mchezo wa Ligi Kuu Tanzania Bara, ambao miamba hiyo ya Jangwani ilipata ushindi wa bao 1-0.

Katika mchezo huo, Yanga ililazimika kusubiri hadi dakika za mwisho kupata bao lililofungwa na mshambuliaji, Amisi Tambwe.

Yanga ilitinga robo fainali, baada ya kuitupa nje timu ya Namungo FC inayoshiriki Ligi Daraja la Kwanza, kwa kuichapa bao 1-0, mchezo uliochezwa Uwanja wa Majaliwa, Lindi.

Kwa upande mwingine, Alliance ilitinga hatua hiyo, baada ya kuiondosha mashindanoni timu ya Dar City inayoshiriki Ligi Daraja la Pili kwa kuitungua mabao 3-0, Uwanja wa Nyamagana, Mwanza.

Akizungumza na MTANZANIA muda mfupi baada ya droo hiyo kufanyika Kocha Mkuu wa Alliance, Malale Hamsini, alidai kufurahia hatua ya kukutanishwa tena na Yanga na kusema amepanga kulipa kisasi.

“Nimepokea kwa mikono miwili matokeo ya droo hiyo, hadi tunafika hatua ya robo fainali tulikuwa tumejipanga kukutana na timu yoyote ile, dhamira yetu ni kushinda na kusonga mbele.

“Yanga walitufunga wiki iliyopita, nafurahi kukutana nao tena, wajiandae  safari hii tunataka kulipa kisasi,” alisema Hamsini.

Mbali na mchezo huo, Azam FC itasafiri mpaka Kagera kuifuata Kagera Sugar  katika mchezo mwingine wa robo fainali utakaochezwa Uwanja wa Kaitaba, Bukoba.

Azam ilitinga hatua hiyo, baada ya kufurusha Rhino Rangers ya Tabora kwa kuichapa mabao 3-0 mchezo uliochezwa  Uwanja wa Azam Complex, Dar es Salaam.

Kagera Sugar ilikata tiketi, baada ya kuizamisha Boma FC kwa kuifunga mabao 2-1, mchezo uliochezwa kwenye uwanja huo.

 Nayo KMC itakabiliana na majirani zao African Lyon Uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam.

KMC ilifika robo fainali baada kuipiga Mtibwa Sugar kwa mikwaju ya penalti 4-3, baada ya kutoka sare 1-1.

Patashika nyingine ya robo fainali itakuwa kati ya Lipuli FC itakayoialika Singida United, mchezo utakaochezwa Uwanja wa Samora, Iringa.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles