27.2 C
Dar es Salaam
Friday, April 19, 2024

Contact us: [email protected]

Kocha Nigeria afurahia sare na Stars

Pg 32*Akiri mambo yalikua magumu upande wao

*Mkwasa asema timu yake imekosa uzoefu tu

NA MWALI IBRAHIM, DAR ES SALAAM

KOCHA Mkuu wa timu ya Taifa ya Nigeria ‘Super Eagles’, Sunday Oliseh, amefurahia matokeo ya suluhu katika mchezo wa kuwania kufuzu kwa fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON) dhidi ya Taifa Stars ya Tanzania, akieleza wazi kuwa maji yalikua shingoni kwa upande wao.

Stars na Nigeria ambazo zimepangwa kundi G kwenye michuano hiyo, juzi zilitoshana nguvu na kuambulia pointi moja katika mchezo uliochezwa kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam wakati Stars ikionyesha kiwango safi tofauti na watu walivyofikiria.

Akizungumza Dar es Salaam mara baada ya mechi hiyo, Oliseh alisema wachezaji wanaounda kikosi chake ni wapya na wamejiandaa kwa siku mbili tu kabla ya kuivaa Stars ndiyo maana wamepata upinzani mkubwa.

“Hatukupata muda wa kutosha kujiandaa na mchezo huu, pia wachezaji wengi ni wapya, lakini nimefurahishwa na kiwango kilichoonyeshwa ila safu ya ushambuliaji ilionekana kuwa butu na kushindwa kuzitumia nafasi walizopata kipindi cha pili, lakini tutafanyia kazi makosa haya.

“Tuligawana mchezo huo, Tanzania walicheza vizuri sana kipindi cha kwanza, sisi tulicheza kipindi cha pili ila wenzetu walicheza vizuri sana hali iliyonifanya nishukuru sare ile kwani mambo yangekuwa mengine ingekua mbaya zaidi, hatukutegemea upinzani tulioupata,” alisema.

Alisema mambo hayakwenda kama walivyokua wamepanga, nafasi ya kiungo ya timu yake katika mchezo huo haikucheza vizuri hali iliyomfanya afanye mabadiliko ya haraka, lakini Kocha huyo alimmwagia sifa golikipa wake, Ikeme Onora anayekipiga katika klabu ya Wolverhampton ya Uingereza.

 

Oliseh ambaye alikuwa akiumiza kichwa kuisoma falsafa ya Mkwasa kabla ya mchezo huo, aliwapongeza Stars kwa kiwango walichoonyesha.

Wakati huo huo Kocha Mkuu wa timu ya Taifa ‘Taifa Stars’, Bonifance Mkwasa, amesema kuwa uzoefu ndio tatizo dogo lililoonekana kuwashinda wachezaji wake, hivyo kushindwa kuibuka na ushindi kwenye mchezo huo.

Mkwasa alisema wachezaji wake wameonyesha mchezo mzuri licha ya kuwa na tatizo la uzoefu, ambapo ni mara yao ya kwanza kucheza na timu kubwa ambayo inarekodi nzuri Afrika kuzidi wao.

Alisema tangu mwanzo waliingia uwanjani kwa tahadhari kubwa kutokana na kufahamu kuwa wanaenda kucheza na timu ya aina gani, hali iliyoifanya timu kushindwa kufunguka mapema wakiogopa ingewagharimu.

“Hawajawahi kuona Nigeria ikicheza ndiyo maana tuliingia kwa tahadhari kubwa na tukaamua kutumia mfumo wa kujilinda zaidi na kushambulia katikati katika kipindi cha kwanza, tuliamua kufunguka kipindi cha pili, tuliogopa kufunguka mapema kwani tungeweza kufungwa,” alisema.

“Hatukupata matokeo ya kuridhisha lakini yanaonyesha mwanga mzuri wa kuwatumia vijana nimefurahi sana, wachezaji wangu wameonyesha mchezo mzuri licha ya kutengeneza nafasi nyingi na kushindwa kuzitumia,” alisema.

Aliwapongeza vijana wake kwa uwezo waliouonyesha na kuyazingatia yale yote aliyowafundisha katika kipindi chote cha maandalizi yao, kuanzia hapa nchini hadi kwenye kambi yao nchini Uturuki.

Mkwasa aliipongeza pia timu ya Nigeria kwa kuonyesha mchezo mzuri, kwani bila wao kufanya hivyo hata wao wasingeweza kufanya vizuri.

 

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles