24.2 C
Dar es Salaam
Thursday, April 25, 2024

Contact us: [email protected]

Kizimbani kwa kuteka na kudai Sh milioni 50 amwachie mateka

Na AVELINE KITOMARY -DAR ES SALAAM 

WATU wawili wamepandishwa kizimbani katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kinondoni, Dar es Salaam kwa shtaka la utekaji. 

Waliofikishwa mahakamani ni Happyness Gimonge (22), mkazi wa Kivule na James Shayo (23), msanii na mkazi wa Kitunda. 

Wakili wa Serikali Abudi Yusuph, alidai mbele ya Hakimu Frank Moshi kuwa Mei 6, eneo la Kimara Bonyokwa, Wilaya ya Ubungo, washtakiwa walimteka Angle Mwita na kumwambia mama yake Christina Massa atume Sh milioni 52 ili kumpata mtoto wake. 

Hata hivyo, washtakiwa kwa pamoja walikana kutenda kosa hilo huku upande wa Jamhuri ulisema upelelezi wa kesi bado haujakamilika. 

Hakimu Moshi alisema shtaka hilo linadhaminika endapo washtakiwa watakuwa na wadhamini wawili wanaotambulika kisheria, watakaotoa bondi ya Sh milioni 5 kwa kila mmoja.

Washtakiwa walishindwa kukidhi masharti ya dhamana na kurudishwa rumande hadi kesi yao itakaposomwa tena Juni 10, mwaka huu. 

Wakati huo huo, mahakama hiyo imempandisha kizimbani Alex Elieza (27), mkazi wa Temeke kwa shtaka la wizi.

Akisoma shtaka hilo mbele ya hakimu Mkazi Karoline Kiliwa, mwendesha mashtaka wa Jamhuri, Neema Moshi, alidai Novemba 23, 2018 eneo la Mbezi Beach, Wilaya ya Kinondoni, mshtakiwa kama mwajiriwa wa Kampuni ya Bevco Distribution Ltd, aliiba Sh milioni 30 na gari lenye namba za usajili MC 377 BFZ aina ya Mahindra mali ya mwajiri wake. 

Mshtakiwa alikana kutenda kosa hilo huku upande wa Jamhuri ukisema upelelezi wa kesi hiyo bado haujakamilika na kuomba tarehe ya kutajwa tena. 

Hakimu Kiliwa alisema dhamana iko wazi kwa mshtakiwa kuwa na wadhamini wawili watakaoweka hati ya mali isiyohamishika yenye thamani ya kiasi cha Sh milioni 30.

Hata hivyo mshtakiwa alishindwa kukidhi masharti ya dhamana na kurudishwa rumande hadi kesi yake itakaposomwa Juni 10, mwaka huu. 

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles