27.2 C
Dar es Salaam
Tuesday, April 16, 2024

Contact us: [email protected]

Kilicho wanyima ubingwa Golden States Warriors hiki hapa

NA BADI MCHOMOLO

NDOTO za timu ya kikapu ya Golden State Worriors kutwaa ubingwa wa Ligi ya Kikapu nchini Marekani (NBA), zilifikia mwisho Ijumaa wiki iliopita katika fainali ya sita.

Golden State Worriors ilifanikiwa kuingia fainali dhidi ya wapinzani wao Toronto Raptors. Katika fainali saba ambazo zilitakiwa kupigwa na kumtafuta bingwa, zilipigwa sita na hatimaye Raptors walitangazwa mabingwa kwenye uwanja wa wapinzani wao huko California nchini Marekani.

Golden State Warriors walikuwa na lengo la kuandika historia ya kuchukuwa ubingwa huo mara tatu mfululizo, lakini Raptors wakizizima ndoto hizo.

Katika michezo sita ya fainali waliyocheza, Raptors imefanikiwa kushinda michezo 4-2, ikiwa michezo mitatu ya ugenini na mmoja wa nyumbani.

Hii ilionesha wazi ni jinsi gani Raptors walivyokuwa kwenye ubora msimu huu hasa kutokana na kiwango cha mchezaji wao Kawhi Leonard ambaye ametajwa kuwa mchezaji bora wa fainali hizo na kutwaa tuzo ya MVP baada ya kujikusanyia wastani wa pointi 28.5.

Kulikuwa na sababu zingine mbalimbali ambazo ziliwafanya Golden State Warriors washindwe kuandika historia hiyo ambazo ni pamoja na;

Majeruhi

Pale Golden State inapokuwa kwenye kiwango bora hasa katika kipindi hiki cha misimu miwili iliopita ni pamoja na uwepo wa kiwango kizuri cha staa wao Stephen Curry, Kevin Durant na wengine.

Uwepo wa wawili hao kuliifanya timu hiyo kuwa bora zaidi na kuwapa mashabiki matumaini ya kuibuka na ushindi kwenye michezo mbalimbali.

Curry ni mmoja kati ya wachezaji ambao wana sifa ya kujikusanyia pointi nyingi kutokana na mitupo yake ya kujipatia pointi tatu.

Amekuwa mzuri wa kujikusanyia pointi tatu kwa kuwa hapendi kushuti akiwa ndani ya eneo la D, hivyo kabla kufika katika eneo hilo anahakikisha anatafuta pointi tatu.

Kwa upande mwingine Durant alikuwa mchezaji wa aina hiyo, hivyo kwa umoja wao uliwafanya kukusanya pointi nyingi kwenye mchezo mmoja na kuifanya timu yao iwe mbele.

Lakini katika michezo sita ya fainali, Golden State ilimkosa Durant katika baadhi ya michezo kutokana na kuwa majeruhi, hata hivyo aliweza kurudi katika mchezo wa tano lakini hakumaliza kutokana na kuchanika nyama.

Kutokana na hali hiyo Curry alikuwa na kazi kubwa ya kufanya ili kuibeba timu hiyo, lakini alikuwa anakutana na ushindani wa hali ya juu.

Kuumia kwa Durant kulimpa nafasi kubwa Klay Thompson ya kwenda kuziba nafasi hiyo, lakini ilikuwa ngumu kufanya kama kile ambacho Durant amekuwa akikifanya.

Hata hivyo mchezo wa fainali ya sita, Thompson hakuweza kuumaliza kutokana na kuumia goti kwenye robo ya tatu ya mchezo.

Matumaini ya Golden kufanya vizuri yaliishia hapo huku Curry akionekana anachuchumaa na kushika kichwa akiamini kuumia kwa mchezaji huyo kutazidi kufanya mambo kuwa magumu zaidi.

Kwa upande mwingine idadi kubwa ya mashabiki walionekana wakishika kichwa na kuudhunika baada ya mchezaji huyo kuumia.

Ubora wa Raptors

Timu ya Raptors ilikuwa na kiu kubwa ya kutwaa ubingwa huo baada ya kushindwa kwa miaka 73 iliopita, hivyo ndoto zao zilikuwa ni kuandika historia mpya.

Hata hivyo, timu hiyo ilikuwa bora msimu huu hasa uwepo wa nyota wao Kawhi Leonard ambaye alitangazwa kuwa MVP msimu huu baada ya Durant kufanya hivyo mwaka jana.

Leonard alikuwa na uwezo wa kuifanya timu kuwa kwenye muanganiko hasa kwenye pointi, alihakikisha anatumia uwezo wake kwa ajili ya kukusanya pointi na kumfanya amalize fainali hizo akiwa na wastani wa pointi 28.5.

Sapoti ya Drake

Huyu ni rapa maarufu nchini Marekani, lakini ni raia wa nchini Canada, hivyo katika fainali hizo hakuweza kuiacha nyuma timu hiyo ya nchini Canada.

Hata hivyo Toronto Raptors waliamua kumpa ubarozi msanii huyo kwa muda mrefu, hivyo alikuwa anatumia nafasi zake kuwapa sapoti mashabiki.

Kuna wakati alishindwa kuzuia hisia zake hasa pale Golden State Warriors walipokuwa wanafanya vizuri kwa kuwa ni shabiki mkubwa wa Stephen Curry na Kevin Durant.

Kwenye mkono wake wa kushoto, msanii huyo amechora tattoo ya namba za jezi za wachezaji hao, hivyo alikuwa anawasifia pale wanapofanya vizuri.

Curry anaamini mchango wa Drake kwa Raptors umechangia kwa kiasi kikubwa wapinzani hao kutwaa ubingwa, hata baada ya kumalizika kwa mchezo nyota huyo aliamua kuchukua simu yake na kumpigia Drake na kisha kumpongeza kwa kile alichokifanya.

Kwa upande mwingine mashabiki wa Raptors huko nchini Canada walitoa sapoti ya nguvu, siku moja kabla ya mchezo huo wa mwisho mjini Toronto idadi kubwa ya mashabiki walikesha kuanza kusherehekea ubingwa, hivyo kitendo hicho kiliwapa nguvu wachezaji na kuamua kupambana kweli.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles