23.2 C
Dar es Salaam
Friday, April 19, 2024

Contact us: [email protected]

KILELEPORI NI MALI YA WANANCHI WA SIHA- CCM

Na SAFINA SARWATT -SIHA

KATIBU wa Itikadi na Uenezi  Taifa wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Humphrey Polepole, amesema eneo la Kilelepori ni mali ya  wananchi wa Siha.

Eneo la Kilelepori limekuwa na mgogoro wa muda mrefu baina ya wananchi na Chuo cha Polisi (TPS) ambapo limekuwa likitumiwa na shule ya taaluma ya polisi kwa ajili ya mazoezi ya kijeshi.

Polepole aliyasema hayo jana kwenye mkutano wa kumnadi mgombea ubunge wa CCM, Dk Godwin Mollel uliofanyika Kata ya Donyomurwak wilayani Siha mkoani Kilimanjaro.

“Nimesema wananchi  wasisumbuliwe tena eneo la Kilelepori ni mali ya wananchi wa Siha, jeshi litafute maeneo mengine kwa sababu wameingilia makazi ya watu,” alisema.

Alisema  kuwa mji unapanuka  hivyo mazoezi hayo ni hatari kuendelea kuwepo kwenye maeneo ambayo tayari kuna watu.

“Nakwenda kuwaagiza mawaziri wa wizara husika ili wananchi wasiendelee kuonewa, serikali ipo kwa ajili ya kutetea wananchi na hatuwezi kuliacha lazima tushughulike nalo,” alisema.

Kwa upande wake, Mollel, alisema endapo wananchi wa Siha watampa kura za kutosha atahakikisha anashughulikia tatizo la umeme, migogoro ya ardhi, barabara,  vifaa vya maabara katika shule za sekondari za kata za serikali na kusambaza maji kwenye Kata ya Donyomurwak.

Naye mgombea udiwani wa kata hiyo, Lwite Ndosi aliahidi kushughulikia tatizo la maji, umeme, pamoja afya. “Naombee sana ndugu zangu nipe ridhaa nikashughulike na matatizo yenu,” alisema Ndosi.

Uchaguzi huo wa marudio unafanyika baada ya wabunge wa Kinondoni, Maulid Mtulia (CUF) na Dk Godwin Mollel (Chadema) kujiuzulu nafasi zao na kujiunga na CCM.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles