27.5 C
Dar es Salaam
Thursday, April 25, 2024

Contact us: [email protected]

KIKWETE APELEKEWA MAJI MSOGA

Na TUNU NASSOR-DAR ES SALAAM


MAMLAKA ya Majisafi na Majitaka Dar es Salaam (Dawasa), imeanza ujenzi wa mradi wa kusafirisha maji kutoka Mlandizi hadi Mboga, Wilaya ya Chalinze mkoani Pwani.

Moja ya vijiji vitakavyonufaika na mradi huo ni Kijiji cha Msoga anachoishi Rais mstaafu Jakaya Kikwete.

Meneja Mawasiliano na Uhusiano wa Jamii wa Dawasa, Neli Msuya, alisema lengo la mradi huo ni kuimarisha huduma ya maji safi katika maeneo yaliyo kati ya Mlandizi na Chalinze kupitia barabara ya Morogoro na ile ya Segera.

“Mradi utawanufaisha wakazi wa 120,912 wa maeneo ambayo bomba litapita, viwanda vilivyopo Chalinze hadi Mboga, ikiwa ni pamoja na Msoga, Bwilingu, Pera, Pingo na Vigwaza.

“Pia utawanufaisha wakazi wa Visenzi, Buyuni, Mdaula Ubenazomozi, Chahua-Lukenge, Chamakweza, Mboga na kiwanda cha vigae cha Twyford na kile cha matunda cha Sayona,” alisema Neli.

Neli alisema mradi huo utatekelezwa kwa miezi saba na tayari kazi mbalimbali zimeanza kufanyika.

“Kazi zilizotekelezwa ni pamoja na upimaji wa njia ya mabomba, usanifu wa mradi, utangazaji na upokeaji wa zabuni ya mabomba na zabuni ya viungio, ambayo itapokewa Juni14, mwaka huu,” alisema.

Neli alisema kazi za uchimbaji mtaro na ulazaji mabomba zitaanza mara baada ya kupokea mabomba.

Alisema mradi huo unatekelezwa kwa fedha za Serikali kupitia bajeti ya ndani ili kupunguza gharama ya kupata thamani ya fedha.

“Mradi utatekelezwa kwa uwezo wa ndani (forced account) ambapo Dawasa ndiye msimamizi mkuu na atakayetekeleza mradi kwa kuwatumia wataalamu kutoka Wizara ya Maji na Umwagiliaji, Shirika la Majisafi na Majitaka Dar es Salaam (Dawasco) na Mamlaka ya Majisafi na Majitaka Chalinze (Chaliwasa),” alisema Neli.

Aliongeza kuwa vifaa muhimu kama mabomba, nondo na saruji vitanunuliwa moja kwa moja kutoka katika viwanda vilivyopo nchini.

“Vifaa ambavyo havitengenezwi nchini kama dira (bulk meters), valvu, valvu za upepo, ‘fire hydrant’ na pampu zitanunuliwa kwa zabuni ya ndani,”  alisema Neli.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles