24.2 C
Dar es Salaam
Thursday, April 25, 2024

Contact us: [email protected]

KIGWANGALA AGOMA WANANCHI KUPEWA ENEO LA HIFADHI

Na DERICK MILTON

WAZIRI wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamis Kigwangala  amemgomea Mbunge wa   Itilima,   Njalu Silanga (CCM), aliyeomba eneo la hifadhi ya Pori la Akiba la Maswa wapewe wananchi wanaopakana na hifadhi hiyo.

Mbunge huyo alimuomba Waziri Kigwangala kukata kipande cha hifadhi hiyo  wapewe wananchi , ambao alidai wamekuwa wakihangaika   kupata maeneo ya malisho   na shughuli nyingine za kilimo na makazi.

Njalu alitoa ombi hilo juzi wakati wa mkutano wa wananchi na waziri huyo katika Kijiji cha Logalombogo kinachopakana na hifadhi ya pori hilo  katika ziara yake ya siku mbili ya kutemebelea maeneo ya hifadhi mkoani Simiyu.

Mbunge huyo alisema   wakati wa kampeini mwaka 2015 Rais  John  Magufuli, aliwaahidi wananchi kuwa atawaongezea eneo kutoka kwenye hifadhi hiyo kwa ajili ya   malisho.

“Hawa wananchi waliahidiwa na Mheshimiwa Rais kuwa atawapatia kipande cha eneo kutoka kwenye hifadhi hii.

“Tnaomba sasa kama mwakilishi wa Rais hawa wananchi waongezewe eneo kwa ajili ya mahtaji yao kutoka kwenye hii hifadhi,” alisema Njalu.

Akitoa majibu ya ombi hilo Dk. Kigwangala alisema  hawezi kukata eneo la hifadhi na kuwapatia wananchi.

Alisema  eneo hilo limekatwa mara nyingi miaka iliyopita na wananchi kupewa lakini bado wameendelea kuomba.

“Kama Rais alisema ni lazima nipate maelekezo kutoka kwake, na akiniambia mimi nakuja kukata maana yeye ndiye mwenye dhamana na mali hizi.

Lakini hajaniambia hivyo siwezi   kukata eneo niwapatie wananchi, hilo siwezi hata kidogo, niwaambie ukweli hakuna eneo watapewa wananchi,” alisema Kigwangala.

Akiwa Busega    Dk  Kigwangala  aliwataka wananchi wa vijiji  vinavyopakana na Hifadhi ya Pori la Akiba   ambao wameanzisha makazi na kufanya shughuli za  jamii kwenye eneo la mita 500 za pori hilo kuondoka mara moja ndani ya   siku 40.

Vilevile alimwagiza Meneja wa Hifadhi hiyo, Diana Chambi kuhakikisha kabla ya siku hizo 40 kuisha, awaandikie barua za kutoka kwenye eneo hilo watu wote waliovamiwa hifadhi hiyo, ikiwa pamoja na kuanza kuweka alama za kutambua mwisho wa hifadhi.

 

“Hapa hakuna utani, hii ni hifadhi tayari kwa hiyo lazima itunzwe na kulinda, tukiwaacha hawa wataendelea na ujangili   na kuchungia mifugo, Septemba mosi  operesheni inaanza kwa mtu atakayegoma kuondoka,” alisema Kigwangala.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles