26.2 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

Kamati Taifa Stars yavunjwa

Jamal+MalinziNA THERESIA GASPER, DAR ES SALAAM

KAMATI ya Timu ya Taifa ya Tanzania ‘Taifa Stars’, jana imevunjwa rasmi baada ya kumaliza kazi yao iliyokuwa inawakabili ya kuhamasisha mechi dhidi ya Algeria.

Kamati hiyo iliyoundwa na Rais wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Jamal Malinzi, ilikuwa na kazi ya kuhakikisha Taifa Stars inafanya vema kwenye michuano ya kuwania kufuzu  kwa kombe la dunia 2018 nchini Urusi.

Akizungumza  jijini Dar es Salaam jana, Mwenyekiti wa kamati hiyo, Farough Baghouzah, alisema kuwa kamati hiyo imevunjwa rasmi kwa kuwa wamemaliza utekelezaji wao.

“Tunawashukuru Watanzania wote  kwa kuweza kusapoti timu yao pamoja na hatua zote tulizopitia, licha ya kutolewa kwa jumla ya mabao 9-2 dhidi ya wapinzani  Algeria,” alisema.

Naye Mlezi wa kamati hiyo ambaye ni Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Said Mecky Sadick, alisema kamati hiyo ilifanya kazi ipasavyo, licha ya kukumbwa na ukata.

Wakati huo huo, Makamu Mwenyekiti wa kamati hiyo, Michael Wambura, alisema kazi kubwa ya kamati hiyo ilikuwa ni kurudisha hamasa kwa mashabiki na morali kwa wachezaji wa timu hiyo.

“Tulianza bila fedha, ndio sababu ya kupitisha harambee ambayo baadaye tulipata Sh milioni 124 kutoka kwa wadau mbalimbali pamoja na mashabiki wa timu hii ambapo fedha hizo ndizo zilitusaidia kufanikisha malengo mbalimbali tuliyojiwekea,” alisema Wambura.

Alisema lengo lao lilikuwa ni kupata Sh milioni 300, ambazo hata hivyo zilikosekana na kupata milioni  124, fedha hizo zilitumika kwa posho za wachezaji, kulipia hoteli, gharama za tiketi za Afrika Kusini walipoweka kambi na Algeria kwenye mechi ya marudiano.

Akifafanua Sh milioni 500 zilizodaiwa kuahidiwa na kamati hiyo kama timu ingefanya vema kwenye michuano hiyo, Wambura alisema fedha hizo hazikuwa kwenye kamati kama ilivyoripotiwa, bali ni ahadi tu iliyotolewa na mashabiki.

“Kwenye mechi ya kwanza iliyofanyika Dar es Salaam kamati iliahadi kutoa milioni 50  kama pongezi kwa wachezaji ambapo baada ya kupata  sare ilibidi wapewe milioni 25,  lakini hizo milioni 500 hazikuahidiwa na kamati bali ni mashabiki tu, walisema watatoa iwapo timu hiyo itafanya vema kwenye mchezo wa marudiano,” alisema.

Akifafanua zaidi, Wambura alisema shabiki mmoja aliahidi atatoa Sh milioni 300, mwingine milioni 100 na Mwenyekiti wa kamati hiyo, Farough milioni 100, ambazo zote zingefika idadi ya Sh milioni 500, lakini fedha hizo hazikutolewa kutokana na matokeo waliyopata kikosi hicho.

Kamati hiyo ya Saidia Stars ilimaliza vema kwa    kuwashukuru wadau mbalimbali, akiwemo Rais Mstaafu Jakaya Mrisho Kikwete, ambaye alitoa Sh milioni 20 kwenye kamati hiyo pamoja na ushauri.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles