26.2 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

KADA CHADEMA AMSHUKIA KATAMBI

Na KADAMA MALUNDE -SHINYANGA

MWENYEKITI wa Baraza la Vijana Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Bavicha) Wilaya ya Shinyanga Mjini, Samson Ng’wagi, amemshukia aliyekuwa mwenyekiti wake taifa, Patrobas Katambi, ambaye amejiondoa chama hicho na kujiunga na Chama Cha Mapinduzi (CCM) kinachomsumbua na kukosa ubunge.

Ng’wagi, ambaye alikuwa Kampeni Meneja wa Patrobas Katambi wakati akigombea ubunge Jimbo la Shinyanga Mjini katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2015, alisema kuhama kwa Katambi kunatokana na hasira ya kukosa uteuzi wa kugombea ubunge wa Afrika Mashariki ndani ya Chadema.

Akizungumza katika kikao na waandishi wa habari juzi, kilichofanyika ofisi za Chadema Kanda ya Serengeti zilizopo mjini Shinyanga, Ng’wagi alisema kiongozi wake huyo wa zamani hana jipya, kwani harakati zake hazikuanza jana wala juzi, ni suala la siku nyingi.

“Harakati za kuondoka Chadema zilikolea hasa alipokosa uteuzi wa kugombea ubunge wa Afrika Mashariki ndani ya chama, alinung’unika sana, kwa kuwa ni rafiki yangu wa karibu niliongea naye na kama haitoshi, nilifika nyumbani kwao na kuzungumza na mama yake, ambaye pia alieleza masikitiko yake kwanini mwanawe hakuteuliwa kugombea nafasi hiyo,” alieleza Ng’wagi.

“Nilishauriana na mama yake tukamshauri Katambi aendelee kubakia Chadema, ingawa baba yake alimtaka aachane na siasa kama haoni maslahi,” alisema.

Alisema hoja za Katambi za ubinafsi, ukabila na ubaguzi ndani ya chama hazina mashiko yoyote, isipokuwa alikuwa na ugomvi wa maslahi binafsi na chama na alishindwa kutambua kuwa Chadema ina watu wengi sana na wenye sifa, uwezo na weledi wa kugombea nafasi ya ubunge wa Afrika Mashariki.

“Lakini pia siyo kweli kwamba Katambi alitumiwa kama karai ndani ya chama chetu, hakuwa karai, alipewa nafasi za juu katika chama, kwani aliaminiwa na kuchaguliwa kuwa mwenyekiti wa Bavicha Taifa na kuwa na sifa ya kuingia kwenye vikao vyote vikuu vya kitaifa,” alisema.

“Kama hiyo haitoshi, alipewa nafasi ya kugombea ubunge Jimbo la Shinyanga Mjini akiwa hana umaarufu wowote ndani ya jimbo na hakuwa na uwezo wa kifedha za kumwezesha kufanya kampeni, hivyo chama kilimpa fedha kwa ajili ya kuendeshea kampeni,” aliongeza.

Alisema kama hiyo haitoshi, Mbunge wa Arusha Mjini, Godbless Lema, alitoa gari lake bila malipo kwa ajili ya Katambi kulitumia katika kufanyia kampeni zake, huku wanachama na wapenzi mbalimbali wa chama wakijitolea kumchangia kumwezesha kufanya kampeni zake.

 

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles