31.7 C
Dar es Salaam
Thursday, March 28, 2024

Contact us: [email protected]

JURGEN KLINSMANN ATIMULIWA KUINOA MAREKANI

U.S, MAREKANI


jurgen_klinsmannSHIRIKISHO la Soka nchini Marekani, limemfukuza kazi kocha mkuu wa timu ya taifa raia wa nchini Ujerumani, Jurgen Klinsmann, baada ya kuifundisha timu hiyo kwa miaka mitano.

Klinsmann mwenye miaka 52, wakati wa ujana wake aliweza kucheza soka la hali ya juu na kufanikiwa kutwaa ubingwa wa Kombe la Dunia, huku akiwa mchezaji wa timu ya taifa ya Ujerumani ambayo iliweza kutwaa ubingwa mwaka 1990.

Rais wa shirikisho hilo, Sunil Gulati, amethibitisha taarifa ya kumfukuza kwa kocha huyo na kudai kuwa hawana wasiwasi wa kufanya vizuri kwa kuwa wana wachezaji wenye kiwango cha hali ya juu ambao wanaweza kufanikisha timu hiyo kufuzu Kombe la Dunia 2018 nchini Urusi.

Rais huyo amedai kuwa wameamua kufanya maamuzi magumu kutokana na mwenendo mbaya wa timu yao, hivyo wameona bora wachukue hatua mapema kwa ajili ya kuilinda timu hiyo iweze kufanya vizuri katika michuano mikubwa.

”Tunaendelea kuwa imara, tuna wachezaji wa kiwango cha juu wa kutusaidia kufuzu Kombe la Dunia mwaka 2018 nchini Urusi, hatuna wasiwasi na maamuzi ambayo tumeyafanya na tunaamini tutapata kocha ambaye ataipeleka timu sehemu ambayo tunaikusudia,” alisema Gulati.

Hata hivyo, kocha huyo ambaye amefukuzwa kazi, alikuwa na mchango mkubwa kwa timu hiyo katika michuano ya Kombe la Dunia 2014, ambapo aliipeleka timu hiyo katika 16 bora  nchini Brazil.

Lakini katika hatua ya kufuzu Kombe la Dunia 2018, walipoteza mchezo wao kwa mabao 2-1 wakiwa kwenye uwanja wa nyumbani dhidi ya Mexico na baadaye walichezea kichapo cha mabao 4-0 dhidi ya Costa Rica. Hali hiyo imewafanya Marekani washindwe kuvumilia na kuamua kumfukuza.

Hadi sasa timu hiyo inashika nafasi ya mwisho katika timu sita kwenye kundi lao, huku timu hiyo ikiwa inawania kufuzu Kombe la Dunia nchini Urusi.

Kutokana na hali hiyo, Marekani imeanza kutafuta kocha ambaye atachukua nafasi ya kocha huyo mapema iwezekanavyo, huku kocha wa klabu ya LA Galaxy, Bruce Arena, amehusishwa kupewa nafasi ya kuwa kocha mkuu.

Awali Klinsmann alihusishwa kutaka kuinoa timu ya taifa ya England mara baada ya kocha Sam Allardyce kujiuzulu Septemba mwaka huu.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles