Mwandishi wetu -Dar es Salaam
RAIS Dk. John Magufuli amepokea hati za utambulisho za mabalozi tisa walioteuliwa kuziwakilisha nchi zao nchini.
Mabalozi waliowasilisha hati zao za utambulisho na nchi zao katika mabano ni Maria Amelia Maio de Paiva (Ureno), Douglas Foo Peow Yong (Singapore), Alex Chua (Ufilipino), Angela Veronica Comfort (Jamaica) na Dk. Christian Fellner (Austria).
Wengine waliowasilisha hati zao za utambulisho ni Francisca Ashietey-Odunton (Ghana), Jesus Agustin Manzanilla Puppo (Venezuela), Yacin Elmi Bouh (Djibouti) na Oded Joseph (Israel).
Kwa mujibu wa taarifa kwa umma iliyotolewa jana na Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, Ikulu, Gerson Msigwa, pamoja na kupokea hati za utambulisho za mabalozi hao, Rais Magufuli alipokea salamu kutoka kwa viongozi wakuu wa nchi hizo, ambao wameeleza kufurahishwa kwao na uhusiano na ushirikiano mzuri na Tanzania, na dhamira yao ya kuukuza na kuuendeleza zaidi uhusiano huo.
Rais Magufuli aliwashukuru viongozi wakuu wa nchi hizo kwa salamu, na amewapongeza na kuwakaribisha mabalozi walioteuliwa kuziwakilisha nchi zao hapa nchini.
Aliwahakikishia kuwa Tanzania ipo tayari kukuza zaidi uhusiano wake na nchi hizo, hasa katika diplomasia ya uchumi, na amewataka kuwahamasisha wafanyabiashara kuja kuwekeza katika sekta mbalimbali, zikiwemo kilimo, ufugaji, uvuvi, madini, mafuta na gesi na biashara nyingine mbalimbali kwa manufaa ya pande zote mbili.
Rais Magufuli alisema anatambua kuwa ushirikiano na nchi hizo utasaidia kubadilishana uzoefu, ujuzi, teknolojia na mitaji itakayosaidia kutumia rasilimali zilizopo Tanzania kwa manufaa ya Watanzania na wananchi wa nchi hizo.