LONDON, England
BONDIA wa uzito wa juu wa IBF na WBA duniani, Anthony Joshua, ametamba kuwa yupo tayari kudundana na mpinzani wake, Deontay Wilder, watakapokutana mapema mwakani.
Hatua hiyo inatokana na kauli aliyotoa Wilder baada ya ushindi aliopata kwa kumdunda Bermane Stiverne. Bingwa huyo wa mkanda wa WBC, alishinda kwa ‘KO’ katika mzunguko wa kwanza katika mchezo uliochezwa Jumamosi iliyopita ambao ulishuhudiwa Stiverne akidondoka mara tatu baada ya kutupiwa konde zito.
Wilder alisema: “Nimekuwa nasubiri kwa muda mrefu kudundana na Joshua, natangaza vita dhidi yake. Utakubaliana na changamoto zangu? Najijua kwamba ni bingwa. Vipi utakubali kujaribiwa?
“Mfalme hafukuzi wakulima. Mfalme anachukua wafalme, Joshua ikiwa hataki kupigana na mimi tutakuwa na mipango mingine. Ulimwengu unamtaka Joshua, ulimwengu unamtaka Wilder, mimi namtaka Joshua.
“Joshua njoo. Haina haja ya kukimbia, haina haja ya kuomba dharura, panga muda haina haja ya kusubiri.”
Joshua ambaye hana rekodi ya kudundwa hada sasa, hakuogopeshwa na vitisho hivyo baada ya kuutambua uzito wa Wilder dhidi ya Stiverne.Uzito wa ngumi ya Joshua ulikuwa nusu ya jiwe wakati alipopigana na Carlos Takam mwishoni mwa wiki iliyopita, huku Wilder akiwa na uzito wa pauni 220.
Lakini alikuwa Eddie Hearn, aliyekatisha pambano la mabondia hao wawili kabla.
Akihojiwa na Sky Sports, Hearn alieleza: “Ni kweli napenda kumshuhudia Wilder akipambana na Joshua. Ningeweza kuruhusu hilo lakini hadi nione utayari wa Joshua, kutokana na utofauti wa uzito, ni kama mawe mawili na nusu kati yao.
“Joshua aliniambia kwamba, tunahitaji mikanda yote, akimaanisha kupigana na mabingwa wa mikanda yote, akiwamo Tyson Fury pamoja na Joseph Parker. “Nilipata ujumbe kutoka kwa promota wa Wilder akihitaji tupange pambano hilo mapema. Kila mmoja anahitaji kupambana na Joshua hivyo tutaona itakavyokuwa baadaye.”