BEKI wa pembeni wa klabu ya Barcelona, Jordi Alba, atakuwa nje ya uwanja kwa siku 10 kutokana na majeruhi aliyoyapata kwenye mchezo wa juzi dhidi ya Athletic Bilbao.
Katika mchezo huo, Barcelona ilifanikiwa kupeleka kilio kwa wapinzani wao baada ya kuwachapa mabao 6-0, ambayo yalifungwa na Luis Suarez mabao matatu, Lionel Messi bao moja, Neymar na Ivan Rakitic wakifunga bao moja moja.
Mchezaji huyo mwenye kasi, aliumia wakati anajaribu kuokoa mpira ambao ulikuwa unatoka nje ya uwanja ambapo alijisababishia maumivu ya nyama za paja.
Hata hivyo, ataukosa mchezo wa kwanza wa robo fainali ya Copa del Rey dhidi ya wapinzani hao, Athletic Bilbao.
Pia mchezaji huyo mwenye umri wa miaka 26, ataanza kurudi uwanjani mwishoni mwa mwezi huu ambapo anaweza kuwa fiti katika mchezo dhidi ya Athletic katika uwanja wa nyumbani wa Camp Nou.
Barcelona kwa sasa wanashika nafasi ya pili katika msimamo wa ligi wakiwa na pointi 45 baada ya kucheza michezo 19, wakati Atletico Madrid wakiongoza wakiwa na pointi 47 baada ya kucheza michezo 20.