27.9 C
Dar es Salaam
Thursday, March 28, 2024

Contact us: [email protected]

Jaji: Kifungo cha Sugu kilikuwa batili

KULWA MZEE-DAR ES SALAAM

MAHAKAMA Kuu ya Tanzania Kanda ya Mbeya,  imetengua hukumu mwenendo na kifungo alichohukumiwa na kukitumikia Mbunge wa Mbeya Mjini, Joseph Mbilinyi maarufu kama Sugu kwa sababu ni batili.

Mahakama hiyo mbele ya Jaji John Utamwa ilitengua hukumu hiyo jana baada ya Sugu kupitia Wakili wake Peter Kibatala na Faraji Mangula kupinga kutiwa hatiani na adhabu aliyopewa na Mahakama ya Hakimu Mkazi Mkoa wa Mbeya.

Itakumbukwa Februari 26 mwaka jana Mbunge huyo wa Mbeya Mjini ‘Sugu’ na Katibu wa Chadema Kanda ya Nyasa, Emmanuel Masonga walihukumiwa kifungo cha miezi mitano jela kila mmoja baada ya kukutwa na hatia kwa kosa la kutumia lugha ya fedheha dhidi ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. John Magufuli.

Hukumu hiyo ilitolewa  na  Mahakama ya Hakimu Mkazi Mkoa wa Mbeya, mbele ya Hakimu Maiko Mteite baada ya kuridhika na ushahidi uliotolewa upande wa mashtaka.

Pia mahakama hiyo ilimuhukumu kifungo cha miezi sita Masonga kwa kosa hilo.

Washtakiwa hao walikuwa wanaotuhumiwa kutenda kosa la kutoa maneno ya kumfedhehesha rais Desemba 31, 2017 katika viwanja vya Luanda Nzovwe wakati wakizungumza na wananchi.

Hata hivyo akisoma uamuzi wa rufaa namba 29 ya Mwaka 2018,  Jaji Utamwa alisema kulikuwa na makosa yasiyothibika katika mwenendo wa shauri hilo,hasa pale ambapo aliyekuwa Hakimu Mwandamizi Mteite wa Mahakama ya Hakimu Mkazi ya Mbeya aliposhindwa kuwasomea Mashtaka Washtakiwa katika hatua ya usikilizaji wa awali (PH).

Jaji Utamwa katika uamuzi wake alisema kwamba hakubaliani na hoja za upande wa Serikali ambao ni wajibu rufaa kwamba mapungufu hayo yanathibitika na badala yake Jaji Utamwa amesema makosa hayo yanaathiri mwenendo mzima wa kesi uliosababisha kufungwa kwa Sugu na mwenzake Emmanuel Masonga.

Kutokana na uamuzi huo Jaji Utamwa ametengua hukumu, mwenendo mzima wa kesi na adhabu ya kifungo waliyohukumiwa Sugu na Masonga.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles