23.7 C
Dar es Salaam
Friday, April 19, 2024

Contact us: [email protected]

Jafo mgeni rasmi uzinduzi jukwa la kilimo

MWANDISHI WETU – DAR ES SALAAM

WAZIRI wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Suleiman Jafo anatarajiwa kuwa mgeni rasmi kwenye hafla ya uzinduzi wa Jukwaa la Kilimo, Kata ya Kurui, Wilaya ya Kisarawe mkoani Pwani.

Katika uzinduzi huo, Jafo ambaye ni kiongozi wa juu wa Serikali katika wilaya hiyo, atakabidhi hatimiliki za kimila za ardhi 315 ambazo zimeandaliwa na Shirika la The Winamwanga Cultural Heritage Association (TWCHA) katika maeneo ya vijiji vya Mafizi, Gwata, Kidugalo, Mtakayo, Zegero na Marui.

Akizungumza katika mkutano wa madiwani na wadau wa maendeleo ya kilimo wakati akitoa taarifa ya kazi zilizofanywa na shirika hilo juzi kwa kipindi cha Novemba na Desemba 2017, Mratibu wa mradi wa kilimo kutoka taasisi hiyo, Saidi Simkonda alisema waliona ni busara Jafo awe mgeni rasmi kwa kuzingatia kuwa yeye ni mwenyeji wa eneo hilo.

 “Tayari mchakato wa kumuomba Waziri Jafo kuwa mgeni rasmi tumeufanya, tunachosubiri ni majibu yake kwani tunapenda kufanya tukio hilo mwanzoni mwa mwezi wa kwanza mwaka 2019,” alisema Simkonda.

Alisema hadi sasa wana wanachama 750, kati ya hao 250 ni walemavu ambao wana mashamba katika kata hizo ambayo yanafanyiwa mchakato wa kupata hatimiliki za kimila za ardhi huku 315 zikiwa tayari.

Simkonda alisema katika kipindi hicho shirika hilo kwa kushirikiana na Halmashauri ya Wilaya ya Kisarawe limeweza kutoa ushauri mbalimbali kwa watu wanaotaka kuendeleza maeneo yao, kufanya mikutano na wananchi juu ya kuwaelimisha namna ya kuipandisha ardhi thamani kwa kupima mashamba yao na kupata hati ya hakimiliki ya kimila.

Alitaja baadhi ya changamoto kuwa ni wananchi wengi wa wilaya hiyo kutokuwa na elimu ya umiliki wa mashamba na umuhimu wa kumiliki haki ya hatimiliki ya kimila na watendaji wa vijiji kutojua makusanyo ya fedha za kodi ya ardhi ya kijiji kuwa zinawakilishwa wapi.

Alisema katika makusanyo ya kodi za ardhi, shirika lilishauri ni vyema kama Serikali za vijiji hazina vitabu vya risiti ni vizuri wananchi wapewe akaunti za Serikali za vijiji kufanya malipo ya tozo za ardhi au makusanyo yoyote kwa maendeleo ya kijiji husika.

Katika mkutano huo madiwani hao waliwakilishwa na Ofisa Kilimo wa Kata ya Kurui, Baraka Mudangi.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles