27.9 C
Dar es Salaam
Thursday, March 28, 2024

Contact us: [email protected]

IPTL yamshtaki Zitto

Zitto Kabwe
Zitto Kabwe

NA MWANDISHI WETU

KAMPUNI ya kufua umeme ya Independent Power Tanzania Limited (IPTL) na wadai wengine wawili, wamefungua kesi ya madai katika Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam dhidi ya Mbunge wa Kigoma Kaskazini,  Zitto Kabwe (Chadema).

Pia IPTL imewafungulia kesi watu wengine wawili, huku wakitaka kulipwa fidia ya Sh. bilioni 500.

Mbali na IPTL, wengine waliofungua kesi hiyo  Septemba 4, mwaka huu kupitia wakili Melchisedeck Lutema wa Asyla Attorneys na  Kay Felician Mwesiga wa Bulwark Associates Advocates, ni Kampuni ya Pan Africa Power Solutions Tanzania Limited (PAP) na Mwenyekiti Mtendaji wa PAP na IPTL, Harbinder Sing Seth.

Wadai hao watatu, miongoni mwa mambo mengine wanahitaji malipo ya fedha kutoka kwa Zitto na washtakiwa wengine watatu akiwamo mhariri wa gazeti la kila siku (sio MTANZANIA) na Kampuni ya Flint Graphics, kuwa kama fidia itokanayo na makala ya kuwachafua iliyochapishwa kwenye gazeti hilo, iliyosababishwa na washtakiwa hao.

Pamoja na hayo, pia wanaomba tamko rasmi kutoka mahakamani, kwamba makala iliyokuwa na kichwa cha habari “Fedha za IPTL ni mali ya umma” iliyochapishwa katika ukurasa wa 7 na 14 wa gazeti hilo la Agosti 13, 2014 ilikuwa ni ya kupotosha na kuchafua kwa kudhamiria.

Pia wanahitaji washtakiwa kuomba radhi kwa kuandika na kuchapisha kurasa za mbele katika matoleo mawili mfululizo ya gazeti hilo.

Wadai hao pia wanaiomba mahakama kuweka vizuizi vya kudumu kwa washtakiwa, watumishi wao, wafanyakazi, washirika, wawakilishi au watu wengine wowote wanaofanya kazi chini yao kwa uchapishaji, kuchapisha au kusababisha kuandika na kuchapishwa makala yoyote ya kuwachafua.

Walisema IPTL waliingia mkataba na Shirika la Usambazaji Umeme Tanzania (Tanesco) kuwa umeme unaozalishwa utakuwa ukinunuliwa na kusambazwa na shirika hilo kwa bei waliyokubaliana.

Inadaiwa  katika kurasa namba 7 na 14 za gazeti hilo  la Agosti 13, mwaka huu, Zitto aliandika, wakati mshtakiwa wa pili wa tatu na wa nne walihariri, kuchapa na kusambaza makala ambayo ilikuwa ni ya uongo na ya kuwachafua wadai.

Katika hati ya mashtaka, wadai walisema makala hiyo ilikuwa na maneno yafuatayo yaliyokuwa si ya ukweli na ya kuwachafua wanaodai; “Kwa mara nyingine, Serikali kupitia viongozi wake akiwamo Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG), wamedai kiasi cha Dola za Marekani milioni 250 zilizopaswa kuendelea kuwapo katika “Tegeta Escrow Account’ si mali ya Serikali na hivyo si mali ya umma.”

Akaunti hiyo ilifunguliwa na Serikali kupitia Wizara ya Nishati na Madini, Tanesco na IPTL.

Ilidaiwa kuwa pasingekuwa na nia ya dhati ya kumchafua  mdai, mdaiwa hasingechapisha, na kusambaza maneno yaliyonukuliwa kama angefanya juhudi za kuthibitisha ukweli kutoka upande wa pili (kwa mdai) au kutoka kwa maafisa husika wa Serikali ambao wangethibitisha kwamba:

“Kiasi cha fedha kilichowekwa kwenye akaunti ya Escrow ilikuwa ni dola za Marekani 122,000,000.00 na siyo dola 250,000,000.00 kama ilivyodaiwa na mshtakiwa,” ilisomeka sehemu ya hati ya madai.

Kwa mujibu wa wadai, Tanesco kamwe haikuwa sehemu ya makubaliano ya Escrow kama ilivyodaiwa na washtakiwa.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles