NEW YORK, MAREKANI
MKUU wa Shirika la kudhibiti uundaji wa silaha za nyuklia duniani amethibitisha kuwa Iran imeongeza uzalishaji wa madini ya uranium ambayo hutumiwa kutengeza silaha za nyuklia.
Mwezi uliopita Iran ilisema itaongeza mara dufu uzalishaji wa madini hayo.
Lakini mkuu huyo wa Shirika la Kimataifa la Nguvu za Atomiki, IAEA,Yukiya Amano, amesema haijabainika wazi kama watafikia kilichokubaliwa katika mkataba wa kimataifa wa mwaka 2015.
Mwezi uliopita Iran pia ilitangaza kuwa itajiondoa katika mkataba wa nyuklia kama hatua ya kulipiza kisasi vikwazo ilivyowekewa na Marekani.
Amano pia amesema anahofu kuhusu taharuki iliyopo sasa kuhusu suala la mpango wa nyuklia wa Iran na kutoa wito wa kufanyika kwa mashauriano.
Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran, Mohammad Javad Zarif baadae alisema hali ya taharuki inaweza kupunguzwa kwa kukomesha kile alichokitaja kuwa “vita vya kiuchumi vya Marekani”.
“Wale wanaoendeleza vita kama hivyo wasitarajie kuwa watakua salama,” aliwaambia wanahabari mjini Tehran wakati wa ziara ya mwenzake wa Ujerumani, Heiko Maas.
Maas alionya kuwa hali katika eneo hilo inaendelea kuwa “tete” na kwamba huenda ikasababisha makabiliano ya kijeshi kati ya Marekani na Iran.
Rais wa Marekani Donald Trump aliindoa taifa hilo katika mkataba wa nyuklia mwaka jana na kuiwekea upya vikwazo iliyokuwa imeiondolea Iran ili kudhibiti shughuli zake za nyuklia.