33.2 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

Google Boy: Mtoto anayeijua Dunia kama kiganja cha mkono

Msanii maarufu nchini India Amitabh Bachchan akiwa na Kautilya Pandit.

Mwandishi Wetu, Dar es Salaam

KATIKA umri ambao kwa kawaida watoto wengi ndio wanajifunza alphabeti hadi maneno, Kautilya Pandit maarufu Google Boy, yeye ni tofauti na wenzake, tayari anajua kila kitu, akitiririka kuanzia Pato la Ndani la Taifa (GDP) la Australia hadi kuzungumzia siasa za Indonesia kwa usahihi kabisa.

Huko Kohand, katika Kijiji cha Karnal, Jimbo la Haryana nchini India, Kautilya tangu akiwa na miaka mitano (2013), tayari alishaanza kujulikana kama ‘Google Boy’ au Encyclopedia inayotembea.

Majina hayo ya utani yanamaanisha kitu chochote ambacho unaweza kukitafuta mtandaoni kama google tayari kipo ndani ya kichwa cha mvulana huyo mwenye umri wa miaka minane.

Wazazi wake wanasema, mtoto huyo tangu akiwa mdogo alikuwa mtu wa kuwarushia maswali ya hapa na pale kuhusu chochote kinachomjia kichwani au kukiona mbele yake.

Kutokana na wakati mwingine kuwatia hofu wazazi wake, walilazimika kwenda kitengo cha saikolojia cha Chuo Kikuu cha Kurukshetra.

Baada ya uchunguzi, waliambiwa IQ ya mtoto wao huyo inasimama katika pointi 130 dhidi ya 92-110 za mtoto wa kawaida na hivyo anapaswa kupewa uangalizi maalumu kielimu.

Kiwango hicho cha IQ ni sawa na kile cha mwanafizikia maarufu Albert Einstein.

“Mtoto huyu mwenye akili Kautilya Pandit, mwenye umri wa miaka mitano tu (2013) anajibu maswali mengi, ambayo wanasayansi na watu wenye maarifa hawawezi kuyajibu,” msanii maarufu nchini India Amitah Bachchan aliandika katika akaunti yake ya Twitter usiku wa Oktoba  25, 2013 baada ya kurekodi kipindi cha televisheni kilichomhusisha Pandit mjini Mumbai.

Katika kipindi hicho, Kautilya aliwashangaza wengi kwa kuchukua sekunde tu kujibu kila swali lililoelekezwa kwake kwa usahihi kabisa.

Kwao Kohand, kwa sasa ni mtu maarufu. “Watu wengi hujitokeza kumtembelea nyumbani kila siku na kupiga naye picha,” anasema baba yake Satish Sharma, ambaye anaendesha shule binafsi kijijini hapo.

Sharma anasema pamoja na kipaji cha mwanawe, ni mtu anayependa kujifunza kila kitu ikiwamo mataifa duniani na ulimwengu kwa ujumla wake.

Yote hayo Sharma anasema alianza kumgundua wakati akiwa na umri wa miaka mitano.

Ilianza kwa yeye kama mwalimu kuwataka na kuwatia moyo watoto wa shule yake wafanye jaribio la kuvunja rekodi iliyowekwa na msichana mmoja mdogo wa Ulaya aliyeweza kuonesha nchi 150 katika ramani ya dunia.

“Niliwataka watoto wote kuleta shuleni atlas ili waweze kufundishwa maeneo ya nchi mbalimbali. Kufikia jioni ya siku iliyofuata, upande wa Kautilya aliweza kuiweka kichwani ramani nzima ya dunia. Siku 20 baadaye aliijua atlasi kama kiganja cha mkono wake,” anasema Sharma.

Shauku ya Kautilya kuifahamu dunia iliyomzunguka iliongezeka kwa kasi, alianza kupitia kwa undani kuhusu nchi moja hadi nyingine bila kuacha miji yao mikuu, chumi zao na kanda zao za kijiografia na hata siasa za ndani za nchi hizo.

Upeo wake ni mkubwa mno kwa kuuliza maswali ya kiutu uzima au kitaalamu kama vile namna ya kuifanya India kuwa taifa kubwa kiuchumi duniani kufikia mwaka 2018 (wakati huo ilikuwa mwaka 2013).

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles