23.3 C
Dar es Salaam
Saturday, April 20, 2024

Contact us: [email protected]

GCLA YASOGEZA HUDUMA MAABARA MBEYA

Na AZIZA MASOUD ALIYEKUWA MBEYA

WAKALA wa  Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali (GCLA) ni taasisi ya  serikali inayojishughulisha na masuala mbalimbali ikiwemo kupima kemikali mbalimbali na  vinasaba vya binadamu (DNA) .

Ofisi  hiyo makao yake makuu yapo Dar es Salaam, kwa sasa imeamua kujitanua katika mikoa kwa mgawanyo wa kikanda lengo ikiwa  kuwafikia wananchi.

GCLA ambayo inaongozwa na Mkemia Mkuu wa Serikali, Profesa Samuel Manyele, imegawanyika katika kanda sita zinazohudumia mikoa mbalimbali.

Kanda hizo ni  kanda ya Kusini  yenye ofisi zake mkoani Mtwara ambayo inahudumia Mtwara na Lindi, Kanda ya Nyanda za Juu Kusini yenye ofisi zake mkoani Mbeya na inahudumia mikoa ya Mbeya, Songwe, Rukwa, Iringa, Njomben Ruvuma na Katavi, nayo ofisi Kanda ya  Kati iliyopo  Dodoma inayotoa huduma Dodoma, Singida na Morogoro.

Mbali na hizo, GCLA ina ofisi katika Kanda ya Mashariki yenye ofisi yake Dar es Salaam  inayohudumia Dar na Pwani wakati Kanda ya Kaskazini inajumuisha mikoa ya Arusha, Tanga, Kilimanjaro na Manyara. Ofisi ya Kanda ya Ziwa iliyopo Mwanza inahudumia Mwanza, Singida, Simiyu, Mara, Tabora, Kigoma na Geita.

Kati ya kanda sita kanda tatu za Kusini, Mashariki na Kanda ya Kati zimeanzishwa katika kipindi cha miaka mitano ya uongozi wa Profesa Manyele.

Katika ofisi zote hizo, wafanyakazi GCLA  wamekuwa wakipewa vyumba vichache  vya kufanyia shughuli zao katika majengo mbalimbali ya Serikali.

Ili kuondoa adha hiyo, Mkemia Mkuu amejenga ofisi ya Kanda ya Nyanda za Juu Kusini Iwambi mkoani Mbeya.

Ujenzi wa ofisi hiyo katika majengo ya hospitali ya Wilaya ya  Mbeya  umegharimu  Sh Milioni 402, fedha zilizotokana na mapato ya ndani ya ofisi hiyo.

Kaimu Meneja wa Kanda hiyo, Gasper Mushi, anasema  jengo hilo katika eneo la Iwambi  lina  lengo la kuboresha shughuli za utoaji huduma za kimaabara zinazofanywa na ofisi hiyo.

“Uwepo wa jengo hili utasaidia kusogeza huduma za kimaabara karibu, mfano  vipo  vipimo ambavyo tunalazimika kuvipeleka Dar es Salaam katika maabara kuu, hii ni kwa sababu tu hatuna eneo la kutosha  la kuhifadhia vifaa vya maabara,” anasema Mushi.

Anasema   usafirishaji wa sampuli za maabara kwenda Dar es Salaam  unasababisha  baadhi ya sampuli kuharibika njiani wakati wa kuzisafirisha.

Mbali ya shughuli hizo, ofisi hiyo pia inajishughulisha na kutoa ushauri wa masuala mbalimbali ya kimaabara.

Jengo hilo jipya ambalo ujenzi wake umeshakamilika, lipo katika taratibu za kuunganishiwa umeme  linatarajiwa kuzinduliwa rasmi  mwakani likiwa na vifaa  mbalimbali vya  maabara ikiwemo mashine ya kupimia vinasaba vya binadamu (DNA).

Anasema kiutaratibu mteja anapaswa kupata majibu ya huduma anayoihitaji ndani ya siku 14  kama hakutakuwa na vikwazo na kama atakuwa amefuata taratibu.

“Sisi tunazingatia mkataba  wa huduma ambao unataka ndani ya siku 14 watu wapate majibu kama taratibu zote zitakuwa zimefuatwa sawasawa hasa katika mazingira ambayo kunakuwa hakuna matatizo ya kiufundi kama ya umeme,” anasema Mushi.

Mganga Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Dk. Seif Mhina, akizungumzia kuhusu umuhimu wa maabara  hiyo, anasema  inasaidia kutatua migogoro mbalimbali inayotokea katika hospitali hizo ikiwemo matukio ya wazazi kubadilishiwa watoto.

“Ofisi inawasaidia wazazi ambao watoto wao wamezaliwa  na utata, wale wenye wasiwasi kwamba huyu mtoto ni wangu au amebambikiwa huwa wanakuja kuhakiki hapa kupimwa kipimo cha DNA.  Wapo wanaobadilisha watoto wanapokuwa wodini  huwa wanakuja kupima kwa kutumia kipimo hicho hicho na wanapata suluhu,” anasema Dk. Mhina.

Anasema mbali na hilo uwepo wa ofisi hiyo katika jengo hilo kunasaidia hospitali kupunguza gharama kutokana na kusaidiana kulipia baadhi ya gharama zikiwemo umeme.

Anasema miaka miwili iliyopita walipatiwa Sh milioni tano kwa ajili ya ujenzi wa barabara za kupitishia wagonjwa.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles