24.2 C
Dar es Salaam
Thursday, April 18, 2024

Contact us: [email protected]

Dk. Tulia sitawaangukia Ukawa

NAIBU Spika wa Bunge, Dk. Tulia Ackson.
NAIBU Spika wa Bunge, Dk. Tulia Ackson.

Na Veronica Romwald, Dar es Salaam

NAIBU Spika wa Bunge, Dk. Tulia Ackson amepigilia msumari wa moto kuhusu kusimamishwa vikao vya Bunge baadhi ya wabunge wa vyama vinavyoundwa na Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa).

Akionekana kujitetea, Dk.Tulia amesema kamwe uamuzi huo haukuwa wa kwake pekee.

Dk. Tulia alikuwa akizungumza katika mahojiano maalumu katika kipindi cha Funguka kinachorushwa kituo cha runinga cha Azam     Dar es Salaam jana.

Alisema uamuzi wa kuondolewa wabunge hao ulifanywa na Kamati ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge.

Alitoa kauli hiyo  wakati  akijibu swali aliloulizwa na mtangazaji wa kipindi hicho, Tido Muhando.

Tido alihoji   mwenendo wa uhusiano uliopo kati yake na  kambi ya upinzani  baada ya kutoa kauli ya kuwafungia kutohudhuria vikao vya Bunge wabunge wake 12.

“Umesema vema, kuna wakati hata bungeni nililazimika kutoa ufafanuzi kuhusu adhabu zinazotolewa, adhabu zilizotolewa bungeni zinazohusu uamuzi wa mimi kukaa pale labda ni tatu, kati ya 12.

“Sasa mjiulize hawa wanaosema nawachukia… kiti kile si cha Dk. Tulia peke yangu, kuna Spika na wenyeviti watatu ambao wanachaguliwa miongoni mwa wabunge wenyewe.

“Adhabu ya kwanza makosa yalifanyika Januari 27, mwaka huu. Si Tulia ambaye alikuwa amekalia kile kiti na wala si yeye aliyeamuru wapelekwe kwenye kamati kuhojiwa,” alisema.

Alisema kiongozi yeyote anayekalia kiti hutoa adhabu chache moja kwa  moja na kwamba nyingi hutolewa na kamati husika  baada ya kupokea mapendekezo.

“Uzuri katika muundo wa kamati, kuna wabunge wa vyama vyote wakiwamo hao wapinzani. Maana yake ni kwamba uamuzi unapotolewa si wangu au wala wa yeyote anayekuwa amekalia kiti kwa wakati huo, ni wa kamati ambayo huwa na wajumbe wapatao 23, sasa wanasemaje nilitoa adhabu hiyo mimi?” alisema.

Dk Tulia alisema uamuzi wa kamati haukutolewa kukandamiza upande mmoja kama wengi wanavyotafsiri.

Alisema hawezi kuzuia mawazo ambayo wengi wamekuwa wakitafakari kuwa huenda amewekwa katika nafasi hiyo kwa ajili ya kudhoofisha upinzani nchini.

“Siwezi kuzuia watu wasiwaze hayo wanayowaza, uamuzi  hautolewi kuegemea upande wowote ule. Bunge linaongozwa kwa kanuni ambazo zimetungwa na wabunge wenyewe.

“Walipeleka hoja kwa Spika ya kuniondoa, tusubiri kamati ipitie hoja yao na kama nilikosea kanuni  wataileta bungeni hoja hiyo ya kuniondoa ipigiwe kura.  Sasa kama idadi yao haitimii itabidi wapate wa kuwaunga mkono katika hilo,” alisema.

Alisema hawezi kusema chochote iwapo anajisikia vibaya au vizuri juu ya uamuzi wa wapinzani kumkataa na akasisitiza kuwa yeye ni kiongozi wa wabunge wote.

“Siwezi kuwazuia wanachofanya, ule ni uamuzi wao kama chama, nitabaki kuwa kiongozi wa wabunge wote… tusubiri uamuzi wa kamati, lakini katika uongozi wa mabunge yote lazima kuwe na changamoto za namna hii. Lazima unapotoa uamuzi kuwe na upande utakaofurahi na utakaohuzunika,” alisema.

Alisema hapendi kuingia katika malumbano yoyote na kwamba anapenda watu wampime kwa utendaji kazi wake.

“Hatua ya kutoka ni uamuzi wao, kila chama kina mikutano yao na inajulikana kwa mujibu wa kanuni, ni mambo ya kawaida na si jambo la ajabu.

“Sijakaa pale kuwakomoa, kanuni zipo wazi… Zinasema Spika ataongoza vikao vya Bunge asipokuwapo atakaa Naibu Spika naye asipokuwapo atakaa mwenyekiti.

“Tatizo ni mazoea yaliyokuwapo, wenyeviti waliachiwa nafasi na ikawa kama desturi tuliyozoea, wanahoji kwa nini wapo, lakini naibu nimekaa, kanuni inaruhusu,” alisema.

Alisema hakupewa nafasi hiyo kama wengi wanavyodhani, kwa sababu   aligombea.

“Nilikuwa na mipango mingine ya maisha, ya kitaaluma, wanasheria wengi wanaingia kwenye siasa   wanapoona muda umefika. Niliona ni wakati mwafaka, nikapima nikaona kwamba hili jambo naweza kulifanya, ndiyo nikachukua hatua.

Siwezi kusema nilipata msaada kupata nafasi hii kwa sababu nilichukua hatua na baada ya kuchukua hatua hiyo mambo mengine yakanikuta njiani, nikateuliwa nashukuru Mungu kwa hayo,” alisema.

Dk. Tulia alikiri kuwa ni mwanachama wa Chama Cha Mapinduzi (CCM)  ingawa hakueleza ni kuanzia kipindi gani.

“Ni kweli nilikuwa Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali, nafasi ambayo niliitumikia kwa kipindi kifupi  nikitokea kwenye kazi yangu ya ualimu pale Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na nilikuwa mwana CCM kwa muda mfupi,” alisema.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles