25.7 C
Dar es Salaam
Friday, April 19, 2024

Contact us: [email protected]

Dk Shein: Hakuna wakuning’oa madarakani

ali-mohamed-sheinNa Mwandishi Wetu, Pemba

MAKAMU  Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) na Rais wa Zanzibar, Dk. Ali Mohamed Shein, amesema   hakuna mtu yeyote mwenye uwezo wa kumwondoa madarakani kwa sababu  yupo kwa mujibu wa sheria.

Alisema  si mwanasiasa wala Jumuiya ya Kimataifa yenye uwezo wa kumwondoa.

Kauli hiyo aliitoa jana Kisiwani Pemba, alipozungumza na watendaji wa chama hicho.

Alisema   licha ya baadhi ya viongozi wa  siasa kuendelea kupotosha na kuwadanganya wananchi,  yeye ndiyo Rais wa Zanzibar aliyechaguliwa kwa mujibu wa sheria.

Alisema uchaguzi wa marudio uliofanyika Machi 20 mwaka huu, ulifanyika kwa uwazi, uhuru na kidemokrasia na katu hakuna njia ya mkato ya kumwondoa madarakani hadi  mwaka 2020.

Kauli hiyo inaelezwa kuwa huenda ni majibu kwa Katibu Mkuu wa CUF, Maalim Seif Sharif Hamad, ambaye katika moja ya mikutano yake alinukuliwa akisema Dk. Shein hatomaliza muda wake madarakani.

Katika kile kinachoonekana kujibu mapigo ya kiongozi huyo wa upinzani mwenye ushawishi mkubwa wa kisiasa Visiwani Zanzibar, Dk. Shein alisema katika dunia ya sasa hakuna kiongozi anayeingia madarakani kwa njia za kuchochea vurugu, mabavu, shutuma na fitna.

Alisema kinachomweka kiongozi katika madaraka ni ridhaa halali ya wananchi kupitia sanduku la kura.

Dk. Shein aliwataka wananchi na watendaji wa chama hicho kujenga utamaduni wa kusoma Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984 ambayo ndiyo mwongozo pekee unaofafanua namna anavyopatikana rais.

“Mkiisoma Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984, ndiyo inayonipa mamlaka ya mimi kuwa Rais kwa sababu nimechaguliwa na wananchi kupitia uchaguzi halali.

“Sasa wanaosema eti hawanitambui basi na wasinitambue kwani Mwenyezi Mungu na Katiba wananitambua,” alisema Dk. Shein.

Alisema ili Zanzibar iweze kuvuka  migogoro na vurugu zisizokuwa za lazima ni lazima iwe na kiongozi wa ngazi ya urais anayejali utu na ubinadamu wa watu wengine na mwenye maono na uvumilivu mpana wa siasa na vigezo ambavyo   yeye   anavyo vyote kama Rais halali wa nchi hiyo.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles