24.2 C
Dar es Salaam
Friday, April 19, 2024

Contact us: [email protected]

Dk. Shein azindua hospitali ya kisasa Pemba

RAIS wa Zanzibar, Dk. Ali Mohamed Shein
RAIS wa Zanzibar, Dk. Ali Mohamed Shein

Na Mwandishi wetu – Pemba

RAIS wa Zanzibar, Dk. Ali Mohamed Shein, amesema uzinduzi wa hospitali mpya na ya kisasa ya Abdalla Mzee, umeandika historia mpya katika utoaji wa huduma za afya kisiwani Pemba.

Amesema kuzinduliwa kwa hospitali hiyo kunaifanya Zanzibar kuwa na hospitali mbili kubwa zinazolingana kiuwezo, huku hatua zikiendelea kuchukuliwa kuimarisha Hospitali ya Mnazi Mmoja kuwa ya rufaa.

Katika hotuba yake akizindua hospitali hiyo iliyoko Mkoani, Mkoa wa Kusini Pemba jana, Dk. Shein alieleza kuwa hospitali hiyo imefikia kiwango cha hospitali ya mkoa kutokana na miundombinu yake, vifaa na wataalamu.

Aliwaeleza viongozi, wageni waalikwa wakiwamo mabalozi na maelfu ya wananchi waliohudhuria sherehe hizo, kuwa hospitali hiyo ina vifaa vyote muhimu vya kisasa vya uchunguzi, huduma na mifumo ya uchunguzi wa magonjwa ambayo haipatikani katika baadhi ya hospitali kubwa nchini.

Alifafanua kuwa hospitali hiyo iliyogharimu shilingi bilioni 35, ikiwa ni msaada kutoka Serikali ya Watu wa China, kutokana na ubora wake haitashangaza watu kutoka nje ya kisiwa cha Pemba kufika huko kufuata matibabu.

Katika hatua nyingine, Dk. Shein amesisitiza kuwa sera ya afya ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ni kutoa matibabu bure kwa kila mwananchi, na kwamba hata pale wananchi wanapotakiwa kuchangia kutokana na upungufu wa baadhi ya nyenzo unaojitokeza baadhi ya wakati, bado si lengo la Serikali kufanya hivyo.

Katika hotuba yake, Dk. Shein aliishukuru Serikali na wananchi wa Jamhuri ya Watu wa China kwa misaada yao kwa Zanzibar na kueleza kuwa miongoni mwa marafiki wa Zanzibar, nchi hiyo ni rafiki wake wa kweli.

Aidha alipongeza kampuni ya ujenzi ya Jiangsu Provincial Construction Group kutoka China kwa kutekekeleza mradi huo kwa kipindi cha miezi 18 kama ilivyopangwa.

Dk. Shein alitoa shukrani pia kwa mabalozi wa China na mabalozi wadogo wa nchi hiyo wa sasa na watangulizi wao kwa kufuatilia kwa makini ujenzi wa hospitali hiyo hadi kukamilika.

- Advertisement -

Related Articles

1 COMMENT

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles