30.2 C
Dar es Salaam
Saturday, April 20, 2024

Contact us: [email protected]

DK. SHEIN AIPONGEZA BENKI YA MAENDELEO AFRIKA

RAIS wa Zanzibar, Dk. Ali Mohamed Shein
RAIS wa Zanzibar, Dk. Ali Mohamed Shein

Na Mwandishi Wetu-Zanzibar

RAIS wa Zanzibar, Dk. Ali Mohamed Shein, amezipongeza juhudi zinazochukuliwa na Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB) kwa kuendelea kuiunga mkono Zanzibar katika kuimarisha sekta za maendeleo.

Hayo aliyasema jana Ikulu mjini Unguja, wakati alipofanya mazungumzo na  aliyekuwa Mwakilishi Mkazi wa AfDB, Dk. Tonia Kandiero, aliyefika Ikulu kumuaga baada ya kupewa majukumu mengine ya kuwa Mkurugenzi Mkuu AfDB kusini mwa Afrika.

Dk. Shein alitumia fursa hiyo kutoa shukurani  zake binafsi kwa kiongozi huyo pamoja na AfDB kwa namna inavyotoa ushirikiano wake kwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kuimarisha miradi ya maendeleo nchini.

Katika mazungumzo hayo, Dk. Shein alieleza kuwa AfDB imekuwa ikichukua juhudi za makusudi katika kuhakikisha miradi mbalimbali ya maendeleo hapa Zanzibar inaimarika na kuendelea kuwasaidia wananchi wote wa Unguja na Pemba.

“AfBD siku zote imekuwa mstari wa mbele katika kuhakikisha Zanzibar inapata mafanikio katika kuendeleza miradi yake mbalimbali ya maendeleo ya kiuchumi na kijamii,” alisema Dk. Shein.

Kwa upande wa uimarishaji wa sekta ya maji katika Mkoa wa Mjini Magharibi, Dk. Shein alieleza kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imefaidika kwa kupata mkopo wenye masharti nafuu kutoka benki hiyo, ambao utasaidia kutatua changamoto ya uhaba wa maji katika mkoa huo na si muda mrefu changamoto hiyo itakuwa historia.

Naye Kandiero alimweleza Dk. Shein kuwa benki yake itaendelea kuiunga mkono Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa kutambua na kuthamini juhudi inazozichukua katika kuleta maendeleo endelevu hapa nchini.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles