26.2 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

Dhamana ya kina Maimu bilioni sita

Aliyekuwa Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (NIDA), Dickson Maimu
Aliyekuwa Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (NIDA), Dickson Maimu

NA VERONICA ROMWALD, DAR ES SALAAM

HATIMAYE Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam imekubali kuwapa dhamana kwa masharti magumu ikiwamo kusaini bondi ya zaidi ya Sh bilioni sita kwa aliyekuwa Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (NIDA), Dickson Maimu na wenzake watano.

Maimu na wenzake wanakabiliwa na mashtaka ya kutumia madaraka vibaya, kula njama, kutumia nyaraka za uongo kumdanganya mwajiri na kuisababishia Serikali hasara ya zaidi ya Sh 1,169,352,931.

Uamuzi huo wa dhamana ambao watuhumiwa wameuhangaikia kwa muda sasa ulitolewa jana mahakamani hapo na Jaji Eliezer Feleshi, baada ya kukamilisha mchakato wa kupitia hoja zilizowasilishwa juzi kwa hati ya dharura na mawakili; Michael Ngalo, Sylvester Kakobe, Seni Malimi, Gordian Isaya Njaala, Audax Vedasto na Godwin Nesphory Nyaisa.

Washtakiwa wengine katika kesi hiyo ni Meneja Biashara, Avelin Momburi,  Kaimu Mhasibu Mkuu wa Nida, Benjamin Mwakatumbula, Mkurugenzi wa Tehama, Joseph Makani, Mkurugenzi wa Kampuni ya Aste Insurance Brokers,  Astery Ndege, Ofisa Usafirishaji,  George Ntalima, Mkurugenzi wa Sheria, Sabina Raymond na Xavery Kayombo.

Kwa upande wake Maimu, Mahakama imekubali kudhaminiwa kwa bondi ya Sh 315,907,061.88 na Dola za Kimarekani 2,172,389.99 au mali isiyohamishika yenye gharama ya kiasi hicho cha fedha kama dhamana yake.

Kwa upande wake, Mwakatumbula dhamana yake ni Sh 105,780,141. 13 na Dola za Marekani 505,723.33 au mali isiyohamishika yenye thamani ya fedha hiyo.

Ndege dhamana yake ni Sh 6,914,100 na Dola za Marekani 33,500 au mali isiyohamishika yenye thamani ya fedha hiyo.

Jaji Feleshi aliamuru, Ntalima kuweka bondi ya Sh 22,056,803. 75 na Dola za Marekani 5,723.33 au mali yoyote isiyohamishika yenye thamani ya kiasi hicho cha fedha.

Naye Raymond ameamuriwa kuweka dhamana ya Sh 225,269,623. 50 au mali isiyohamishika sawa na kiasi hicho wakati Kayombo akitakiwa kuweka dhamana ya Sh 7,585,993.50 au mali isiyohamishika yenye thamani hiyo.

Jaji Feleshi alidai kwamba kila mshtakiwa anatakiwa kutekeleza masharti ya dhamana kwa kulipa nusu ya kiasi anachodaiwa kuitia hasara Serikali na kuwa na wadhamini wawili ambao watasaini bondi hiyo.

Mbali na sharti hilo la dhamana washtakiwa pia watatakiwa kuripoti kila Jumatatu kabla ya saa sita mchana katika Ofisi za Makao Makuu ya Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru).

Sharti lingine ni kwamba kila mshtakiwa hana ruhusa ya kusafiri nje ya Mkoa wa Dar es Salaam bila kupata idhini ya Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu.

Jaji Feleshi alisema ni lazima pia kila mshtakiwa kusalimisha mwenyewe kwa Takukuru hati yake ya kusafiria na nyaraka nyingine yoyote ya kusafiri kama anayo.

Wakili wa washtakiwa hao aliieleza mahakama kuwa wateja wake wanao wadhamini wa kuaminika na kwamba watatoa ushirikiano kwa Takukuru wakati wote wa uchunguzi.

Agosti 17, mwaka huu Maimu na wenzake walifikishwa kwa mara ya kwanza katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu wakikabiliwa na mashtaka 27.

Hadi gazeti hili linaondoka mahakamani hapo jana washtakiwa hao walishindwa kukamilisha mchakato wa masharti hayo ya dhamana.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles