27.5 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

DENI LA TAIFA LAPANDA

 

Na ESTHER MBUSSI-DODOMA


DENI la Taifa limezidi kupanda ambapo kwa sasa limefikia Dola za Marekani milioni 26,115.2 ( zaidi ya Sh trilioni 58) hadi kufikia Juni 2017,  sawa na ongezeko la asilimia 17.0, ikilinganishwa na dola milioni 22,320.76 (zaidi ya Sh trilioni 50) katika kipindi kama hicho mwaka 2016.

Fedha hizo za Tanzania ni kwa mujibu wa viwango vya kubadilisha fedha za kigeni vya Benki Kuu (BoT) jana, ambavyo vilionesha dola moja ni sawa na Sh 2,224.85

Ongezeko hilo lilichangiwa na mikopo mipya iliyochukuliwa ili kugharimia miradi ya maendeleo kama vile Reli ya kisasa ya Standard Gauge, Miji ya kimkakati, mradi wa usafirishaji Dar es Salaam (DART) na kupanua upatikanaji wa maji safi Dar es Salaam.

Hayo yalisemwa bungeni mjini Dodoma jana na Waziri wa Fedha na Mipango, Dk. Philip Mpango, alipokuwa akiwasilisha Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa mwaka wa fedha 2018/19 na maandalizi ya mpango wa bajeti 2018/19, ambapo alisema kupanda huko kwa deni hilo la Taifa kunajumuisha deni la Serikali lililofikia dola za Marekani milioni 22,443.70 (zaidi ya Sh trilioni 50) na deni la sekta binafsi la Dola za Marekani milioni 3,671.50 (zaidi ya Sh trilioni 8).

“Pamoja na ongezeko hili, viashiria vyote bado vinaonesha kuwa deni la Taifa ni himilivu kwa kipindi cha muda mfupi, wa kati na mrefu huku uwiano kati ya deni na Pato la Taifa umefikia asilimia 31.2 ikilinganishwa na ukomo wa asilimia 56,” alisema.

MFUMUKO WA BEI

Alisema mfumuko wa bei bado umeendelea kubakia katika wigo wa tarakimu moja kutokana na kuongezeka kwa ugavi wa chakula katika masoko ya ndani na ya nchi jirani na  kutoyumba kwa bei za mafuta ya petroli katika soko la dunia sambamba  na utekelezaji wa sera za bajeti za kupunguza matumizi yasiyo na tija.

“Mfumuko wa bei mwezi Julai ulikuwa asilimia 5.2, Agosti asilimia 5.0 na Septemba asilimia 5.3 ikilinganishwa na lengo la asilimia 5 hadi 8 kwa kipindi husika. Mwenendo wa Thamani ya Shilingi ya Tanzania dhidi ya dola ya Marekani uliendelea kuwa imara katika kipindi chote cha mwaka 2016/17 narobo ya kwanza ya 2017/18.

“Thamani ya shilingi ya Tanzania imebadilika kutoka shilingi 2,177.26 kwa dola moja ya Marekani mwezi Januari 2016, hadi shilingi 2,221.96 mwezi Januari 2017,” alisema Dk. Mpango

THAMANI YA SHILINGI

Waziri huyo wa fedha alisema kasi ya shilingi kupungua thamani iliongezeka na kudumu kwa muda mfupi mwezi Januari 2017 hali iliyosababishwa na Benki Kuu ya Marekani kupandisha riba yake na hivyo kuongeza mahitaji ya dola ya Marekani duniani kwa ajili ya kuwekeza.

Alisema baada ya Januari 2017, thamani ya shilingi iliendelea kuwa tulivu na kufikia shilingi 2,237.78 Oktoba mwaka huu.

MAPITIO YA BAJETI 2016/17

Alisema Serikali ilitekeleza bajeti kulingana na upatikanaji wa mapato, ambapo yaliyopatikana kutoka vyanzo vyote kwa mwaka 2016/17 yalikuwa Sh bilioni 23,634.55, ikilinganishwa na  makadirio ya Sh bilioni 29,539.60.

Alisema mapato ya ndani yalikuwa Sh bilioni 16.639, sawa na asilimia 90.2 ya makadirio lakini yakiwa na ongezeko la asilimia 17.7 ikilinganishwa na makusanyo ya mwaka 2015/16.

MISAADA

Alisema misaada na mikopo nafuu kutoka kwa washirika wa maendeleo ilifikia Sh bilioni 2,474 sawa na asilimia 68.7 ya ahadi.

Kati ya fedha hizo mikopo ya ndani ilikuwa Sh bilioni 4,504.8 sawa na asilimia 83.8 ya lengo la kukopa Sh bilioni 5,374.3.

Alisema kwa upande wa mikopo ya nje ya kibiashara, Sh bilioni 1,226.8 zilipatikana, ikiwa ni asilimia 58.4 ya malengo ambapo Sh bilioni 1,211.0 kati ya mikopo yenye masharti ya kibiashara hakikuweza kutumika kwa mwaka 2016/17 kwa kuwa kilipokelewa mwishoni mwa mwaka.

Alisema fedha hizo zitatumika kugharamia miradi ya maendeleo iliyokusudiwa katika mwaka 2017/18.

Dk. Mpango alisema ili kukabiliana na changamoto hizo Serikali inachukua hatua madhubuti ikiwamo kuimarisha mifumo ya taasisi za ukusanyaji mapato, kuimarisha ulinzi wa rasilimaali za taifa na kuendelea na zoezi la utambuzi na usajili wa  mapato.

Katika mpango mpya wa maendeleo, Dk. Mpango ameainisha vipaumbele na miradi itakayopewa msukumo wa pekee kuwa ni pamoja na viwanda, mradi waa makaa ya mawe Mchuchuma, Kiwanda cha kufua mawe cha Liganga, shamba la miwa na Kiwanda cha Sukari Mkulazi.

“Katika kulipa na kuzuia ongezeko la madeni ya serikaali, Maofisa Maasuuli wanaagizwa kuhakikisha madai yote yamehaakikiwa na Mkaguzi wa Ndani wa Serikali na kuingizwa kwenye hesabu za fungu husika,” alisema

MAOTEO YA BAJETI 2018/19

Alisema kwa kuzingatia sera za uchumi jumla pamoja na misingi na sera za bajeti kwa mwaka 2018/19, maoteo ya awali yanaonesha kuwa jumla ya Sh bilioni 32,476 zinatarajiwa kukusanywa na kutumika katika kipindi hicho.

“Maoteo haya yatathibitishwa baada ya kufanya uchambuzi wa mwenendo wa utekelezaji wa bajeti katika kipindi cha nusu  ya kwanza ya mwaka 2017/18. Mapato ya ndani yanatarajiwa kuwa shilingi bilioni 22,088.2, sawa na asilimia 68 ya mahitaji yote.

“Kati ya hayo, maoteo ya mapato ya kodi yatakuwa Shilingi bilioni 18,817.0 sawa na asilimia 85.2 ya mapato ya ndani. Vile vile, mapato yasiyo ya kodi yatakuwa Shilingi bilioni 2,423.5 na mapato kutoka vyanzo vya Halmashauri yatakuwa Shilingi bilioni 847.7.

“Serikali inategemea kukopa kiasi cha dola za Marekani milioni 600 sawa na shilingi bilioni 1,374.0 kutoka vyanzo vya nje vyenye masharti ya kibiashara na shilingi bilioni 4,028.6 ni mikopo ya ndani kwa ajili ya kulipia hatifungani na dhamana za Serikali zinazoiva.

“…aidha, Shilingi bilioni 1,327 sawa na asilimia 1 ya Pato la Taifa, itakuwa ni mikopo mipya ya ndani kwa ajili ya kugharamia miradi ya maendeleo,” alisema

Dk. Mpango alisema mwongozo wa maandalizi ya Mpango na Bajeti kwa Mwaka 2018/19 na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka 2018/19 yanalenga  kujenga uelewa wa pamoja juu ya hali ya uchumi na utekelezaji wa bajeti na miradi ya maendeleo kwa mwaka wa fedha uliopita.

KAMATI

Akiwasilisha taarifa ya Kamati ya Bajeti, Mwenyekiti wa Kamati hiyo,  Hawa Ghasia alisema mwongozo wa Dk. Mpango haujaweza kutoa ufumbuzi wa kutatua changamoto ya upatikanaji wa fedha kutoka kwa wafadhili ambazo kwa kiasi kikubwa huelekezwa kwenye utekelezaji wa miradi ya maendeleo.

“Takwimu zinaonyesha utekelezaji wa miradi ya maendeleo kwa kipindi cha bajeti ya mwaka 2016/17 haukuwa wa kuridhisha, hali iliyosababisha serikali kutumia baadhi ya fedha zake za ndani ambazo zilitengwa kwa ajili ya matumizi yaa kawaidaa kugharamiaa miradi hiyo.

“Hatua hii itasababisha serikali kuzalisha madeni ya wakandarasi wa ndani hasa kwa matumizi ya kaawaidaa ambayo si lazima yafanyike.

“Kamati inaatoaa angalizo fedha zinazokopwa zielekezwe katika utekelezaji wa miraadi ya maendeleo ya kimkakati itakayoleta matokeo chanya na ya haraka kiuchumi,” alisema.

Pamoja na mambo mengine, Ghasia alisema mwenendo wa serikali kukopa zaidi ya vyanzo vyake vya ndani kwa ajili ya kuziba nakisi ya bajeti unaathiri zaidi ukuaji wa sekta binafsi ambapo pia mwongozo huo haujatoa ufafanuzi wa kutosha kuhusu uimarishaji naa ukuaji wa sekta binafsi kupitia upatikaanaji wa mitaji katika vyombo vya fedha vya ndani.

KAMBI YA UPINZANI

Akiwasilisha maoni ya Kambi ya Upinzani, Msemaji wa Kambi hiyo kwa Wizara ya Fedha na Mipango, David Silinde, alisema kuna baadhi ya miradi ya maendeleo inatekelezwa nje ya bajeti na hawajaona serikali ikiomba bajeti ya nyongeza katika kutekeleza miradi hiyo.

“Kwa mfano mradi wa mradi wa umeme wa Stiggleres Gorge, ujenzi wa barabara za juu Dar es Salaam, ujenzi wa mabweni Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) ni baadhi ya miradi ambayo bajeti zake haziko bayana.

“Kitendo chaa serikaali kuaamuaa kufaanya re-allocation ya bajeti bila kupata idhini ya bunge ni dharau kwa bunge lakini mbaaya zaidi ni uvunjaji wa sheria na katiba,” alisema Silinde.

Silinde alisema serikali pia imekuwa haionyeshi uwezo wa kuziwezesha sektaa binaafsi kukua ili ziweze kuipunguziaa serikali mzigo mkubwa wa mamilioni ya Watanzania wasio na ajira.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles