23 C
Dar es Salaam
Saturday, April 20, 2024

Contact us: [email protected]

DC: Sikuteuliwa kuongoza makaburi

mgandilwaNa NORA DAMIAN – DAR ES SALAM

VIFO vya waendesha pikipiki   (bodaboda) vimemtisha Mkuu wa Wilaya ya Kigamboni, Hashim Mgandilwa.

Amesema  hataki kuendelea kuvisikia kwa sababu  hakuteuliwa kuongoza makaburi.

Kwa mujibu wa mkuu huyo, kila siku waendesha bodaboda kati ya mmoja hadi wawili wanafariki dunia huku sababu kubwa zikiwa ni uzembe wao na kutozingatia sheria za usalama barabarani.

Akizungumza juzi wakati wa kupanda miti katika wilaya hiyo, Mgandilwa alisema kuna ongezeko kubwa la ajali za barabarani linalosababisha vifo hivyo ingawa nyingi zinaweza kuzuilika.

“Kila siku dereva mmoja wa bodaboda anafariki dunia.  Juzi (Alhamisi) walikufa  wawili, jana (Ijumaa)  mmoja.

“Hatutaki tuongoze makaburi tunahitaji tuongoze watu, wao kama hawajithamini sisi tunawahitaji na tutatumia nguvu zetu kuhakikisha tunaendelea kuwatunza,” alisema Mgandilwa.

Aliliomba Jeshi la Polisi kuongeza askari wa usalama barabarani kudhibiti matukio ya ajali ambayo yanaendelea kuongezeka kila siku na kugharimu maisha ya Watanzania wengi na wengine wakibaki na ulemavu.

Kuhusu   upandaji miti, aliwataka watendaji wa wilaya hiyo kuhakikisha miti yote iliyopandwa inatunzwa vizuri  isikauke.

Naye Diwani wa Kata ya Vijibweni ambaye pia ni Meya wa Jiji la Dar es Salaam, Isaya Mwita, aliwashauri watendaji wa halmashauri hiyo kuendelea kuwa wabunifu kuhakikisha Kigamboni inapata maendeleo.

Awali, Mkurugenzi wa Halmashauri hiyo, Stephen Katemba, alisema katika hatua hiyo miti 5,000 ilipandwa katika maeneo mbalimbali ya wilaya hiyo.

“Watendaji wote wa kata muhakikishe miti iliyopandwa haikauki na mtanipa utaratibu miti iko wapi   niwe napita kuikagua,” alisema Katemba.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles