25.2 C
Dar es Salaam
Thursday, April 25, 2024

Contact us: [email protected]

DC ATAKA SUNGUSUNGU KUSHIRIKISHWA MIRADI

Na KADAMA MALUNDE

MKUU wa Wilaya ya Shinyanga, Josephine Matiro amezitaka taasisi na mashirika yasiyokuwa ya  serikali yanayotekeleza miradi ya maendeleo katika jamii kushirikiana na   sungusungu, viongozi wa  mila na watu maarufu katika maeneo husika  kufanikisha miradi yao.

Matiro aliyasema hayo   mjini Shinyanga wakati akizindua mradi wa kuzuia ukatili wa  jinsia kwa watoto na wanawake.

Mradi huo  unatekelezwa na Shirika la lisilokuwa  la serikali la The Voice of Marginalized Community (TVMC) linalotoa huduma za  jamii kwa vijana, watoto na wanawake na makundi yasiyojiweza.

Matiro alisema taasisi na mashirika mengi yamekuwa yakijisahau kushirikisha viongozi  wa sungusungu, viongozi wa  mila na hata watu maarufu wakati wa kutambulisha miradi mbalimbali katika jamii.

“Pamoja na kuwapa kipaumbele viongozi wa dini bado mnasahau kushirikisha makundi mengine muhimu kama   sungusungu ambao wana nguvu kubwa katika jamii, mkitaka kufanikiwa zaidi washirikisheni watu hao,”aliongeza Matiro.

Aliyataka mashirika yanayotekeleza miradi ya maendeleo kujitambulisha katika jamii badala ya kuanza kutekeleza miradi yao kimya kimya   kuepusha migogoro inayoweza kujitokeza katika jamii.

“Serikali ipo nanyi bega kwa bega, mnapokwama tafadhali tupeni taarifa nasi tutawasaidia kadri tutakavyoweza kwa sababu  lengo kuu ni kuwahudumia wananchi wetu   kuzuia vitendo vya ukatili wanavyofanyiwa wanawake na watoto katika jamii,”aliongeza Matiro.

Awali   Mkurugenzi wa TVMC, Mussa Ngangala alisema mradi huo   unaolenga kupiga vita vitendo vya ukatili wa  jinsia utatekelezwa katika kata tano katika wilaya ya Shinyanga ambazo ni Usanda, Samuye, Nsalala, Tinde na Didia.

Ngangala alisema ili kutekeleza mradi huo kwa ukamilifu shirika hilo litashirikiana na wadau mbalimbali wakiwamo viongozi serikali, dini, wananchi na wadau wengine.

“Matarajio yetu kupitia mradi huu ni kwamba kufikia  Januari mwaka 2018 kuwapo   mfumo mzuri wa kutoa taarifa za ukatili wa kijinsia kutoka ngazi ya jamii hadi dawati la jinsia kwa kushirikiana na maofisa utamaduni,   watendaji, maofisa maendeleo ya jamii, ustawi wa jamii na mashirika mengine,”alieleza Ngangala.

Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi TVMC, Japhet Daud alisema kupitia mradi huo itaibuliwa mijadala kuhusu vitendo vya ukatili wa  jinsia kupitia matamasha, michezo, ngoma za asili, kutoa elimu na mbinu nyingine kadha wa kadha.

 

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles