27.9 C
Dar es Salaam
Thursday, March 28, 2024

Contact us: [email protected]

DC aagiza silaha za mmiliki wa shule zichunguzwe 


ELIYA MBONEA-ARUSHA

VYOMBO vya ulinzi na usalama wilayani Arumeru, Mkoa wa Arusha, vimeagizwa kufanya ukaguzi wa vibali vya silaha tatu za mmiliki wa Shule ya USA River Academy, anayedaiwa kuwafyatulia risasi walimu na kuwajeruhi.

Agizo hilo lilitolewa wilayani hapa jana na Mkuu wa Wilaya ya Arumeru ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Ulinzi na Usalama, Jerry Muro.   

Akielezea kuhusu tukio hilo, Muro alisema mtuhumiwa bado anaendelea kushikiliwa na Jeshi la Polisi wilayani humo kwa mahojiano zaidi.

Alisema kwamba, katika hatua za awali wamemkuta mmiliki huyo anayedaiwa kujeruhi walimu wake wawili waliokuwa wakidai mishahara akimiliki silaha tatu za aina tofauti.

“Kamati ya ulinzi na usalama, iliagiza silaha aina ya shortgun inayodaiwa kutumika eneo la tukio, ipatikane na nimeelekeza ifanyiwe uchunguzi wa kitaalamu.

“Pia, amekutwa akimiliki silaha nyingine aina ya bastola na bunduki aina ya rifle. Lipo swali la kujiuliza kwanini mtu mmoja awe na bunduki tatu?

“Je, yeye ni jeshi au kampuni ya ulinzi binafsi, kwanini amiliki bunduki zaidi ya mbili. Napaswa kuwa na majibu sahihi kwa sababu mimi ndiye Mwenyekiti wa Kamati ya Ulinzi na Usalama.

“Suala la kutambua anamiliki silaha tatu kihalali au si kihalali, tunaendelea kulifanyia kazi na nimeagiza uchunguzi ufanyike wa kupitia vibali kama anavyo na kuvikagua.

“Pamoja na hayo, anayemiliki silaha zaidi ya moja, kamati ya ulinzi na usalama Wilaya ya Arumeru, tutahitaji kukaa na kuzungumza naye,” alisema Muro.

Akitoa tahadhari kwa wamiliki wote wa silaha wilayani hapa, Muro aliwataka warejee kanuni na taratibu walizokabidhiwa wakati wa kupewa silaha zao.

“Unapopewa silaha kwenye kitabu kuna maelezo na miongozo ya umiliki wa silaha, silaha si kwa ajili ya mbwembwe, kuonyeshea watu, kujitamba na kufyatulia makufuli ya mageti.

“Arumeru ukikiuka matumizi ya silaha, tutaichukua silaha yako na kuihifadhi mpaka hapo tutakapothibitisha akili yako imekaa sawa,” alisema Muro.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles