27.5 C
Dar es Salaam
Thursday, April 25, 2024

Contact us: [email protected]

DANGOTE KIWANDA KITAMSHINDA KWA MATATIZO

Na Mwandishi Wetu

Mtengenezaji Saruji wa pili barani Afrika, Dangote Cement, katika kiwanda chake cha Mtwara mambo si kuntu kwani kimejaa matatizo mengi yanayotokana na uongozi mbovu na aina isiyozoeleka ya menejimenti yake ambayo huwaacha wafanyakazi na wateja hoi kwa sintofahamu  na changamoto  nyingi.

Mmiliki wake, Aliko Dangote, tajiri namba  moja  barani Afrika kwa kuwa na utajiri wa dola bilioni 12, haijulikani aliko  lakini akija huwa kama mtalii kwani ana shughuli nyingi za  kiuchumi sehemu mbalimbali duniani na kuufanya uwekezaji wake huo wa dola milioni 600 ulioanza uzalishaji Juni mwaka jana uonekane hauna uzito kwake kwani yupo na hayupo kiutendaji.

“Kiwanda hicho kimekuwa kama gari bovu kwani kila baada ya miezi mitatu kinafunga shughuli za uzalishaji kutokana na sababu moja au nyingine  na kuendeshwa kiujanja  ujanja, ambapo kampuni hiyo haitaki kubeba majukumu ya msingi ya mwenye mali na uzalishaji bali hutumia watu wa tatu kufanya kazi na yeye kusubiri faida yake na hivyo kukwepa hasara na matatizo ya wafanyakazi,” kinasema chanzo chetu cha habari ndani ya kampuni hiyo na hivyo kufanya wafanyakazi kuchoka na mwenendo wa kampuni uliojaa sintofahamu nyingi na mwenye mali asiye kuwepo.

Habari za kuaminika kutoka kiwanda hicho, zinadai kuwa Dangote  amekodisha suala la ajira kwa kampuni binafsi na vilevile usafirishaji na uendeshaji kiwandani, kwani wafanyakazi wake hawakuajiriwa moja kwa moja na Dangote na hivyo kukwepa matatizo ya kila siku ya uwajibikaji na utendaji.

“Anachohitaji yeye ni saruji yake na hiyo haiuzi mwenyewe ila kwa mnunuzi wa jumla wa Kichina ambaye  ndio soko lake na huwauzia watu wengine saruji hiyo, wakati mwingine bei ya chini kuliko ile inayouzwa  na Dangote mwenyewe anapojisikia kufanya hivyo.

“Kampuni hiyo imewashangaza wengi kwani hata lile eneo la madini ya makaa  ya mawe  alilopewa na Wizara ya  Nishati na  Madini kwa maagizo ya  Rais John Magufuli   analitafutia  mnunuzi  ili Dangote anunue makaa kutoka kwake na  si kuchimba makaa, kwani anaona ni  hatari na hakuna faida,” anaeleza mtoa habari wetu.

“Dangote amemchezea shere Rais Magufuli  kwani yeye hayuko vile raisi anavyomfikiria, kwani  huwa hataki uwajibikaji mkubwa sana bali  apate faida kubwa katika shughuli zake,” anatutonya.

Anasema hata wakati  anaposimamisha  uzalishaji, hufanya hivyo si kwa kuharibika mitambo bali ni  njia mojawapo ya  kutaka kuongeza bei kwa  kuanzisha uhaba usiokuwepo na hivyo kufanya kiwanda chake kisiaminike na wafanyabiashara  wakubwa kwa kukosa uhakika wa uzalishaji  saruji na kuwepo na wahusika wengi mno. Katika kiwanda hicho wanaofanya maamuzi ni wengi na hivyo kukosa  mlolongo wa madaraka na hivyo kutokujulikana  nani  ni nani, kwani kila ofisa kuonekana kuwa na madaraka.

Rais Magufuli akiwa ziarani Mtwara, alitembelea kiwanda hicho ambacho ilidaiwa kuwa kinahitaji makaa ya mawe kwa ajili ya uzalishaji  saruji na kuungiwa bomba la gesi asilia ili nalo lisaidie uzalishaji wake  kwa kuuziwa kwa bei poa na Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC), kwani lilipanga kumuuzia kwa bei ya Dar es Salaam, kitu ambacho Dangote alikataa  na hivyo kukiweka kiwanda katika hali mbaya ya  upatikanaji  wa nishati yake kwa uzalishaji na kuzalisha  umeme kwa matumizi ya kiwanda kwani uliopo hautoshi kwa kuendesha mitambo yote.

Rais Magufuli  alikubaliana na Dangote  na kufanya maamuzi magumu ambayo  yalizua lawama  kwa wazalishaji wengine wa  saruji nchini.

Rais  Magufuli aliiamuru TPDC kumuunganishia  Dangote gesi asilia kwa gharama zake na kuiuza kwa bei ya chini ya ile ya Dar es Salaam kama motisha ya kuwekeza Mtwara  na vilevile aliiagiza Wizara kumpa Dangote  eneo la kuchimba makaa ya mawe   yake mwenyewe huko Mbinga  na yote haya yalitekelezwa, lakini hakuna maendeleo kwa upande wake Dangote na hali imeendelea kuwa mbaya kiwandani na kufungwa kiwanda hicho kwa kile kinachosemekana kukosa makaa ya mawe wakati kule Mbinga yanatafuta watumiaji na wanunuzi baada ya  kuwekeza kwa kuboresha mitambo na kupata viwango kutoka kwa Shirika la Viwango Tanzania (TBS) ya mwenendo wa biashara hiyo.

Dangote anaamini  kuwa ushindani ni kitu kizuri na ndio unaofanya biashara isonge mbele na kupunguza gharama za uendeshaji.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles