24.1 C
Dar es Salaam
Friday, April 19, 2024

Contact us: [email protected]

DAKTARI BINGWA WA MOYO JKCI ATUMBULIWA

NA VERONICA ROMWALD – DAR ES SALAAM


UONGOZI wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI), umemfukuza kazi

mtumishi wake, ambaye ni daktari bingwa wa magonjwa ya moyo, Benadetha

Kemilembe kwa kosa la utovu wa nidhamu.

Mkurugenzi Mtendaji wa JKCI, Profesa Mohamed Janabi, alisema hayo jana

alipozungumza wakati alipokuwa ‘akiwafunda’ watumishi wapya 57 walioajiriwa hivi karibuni na taasisi hiyo.

“Sisi ni madaktari, kazi yetu inahitaji nidhamu kwa sababu tukikosea tu, tunakuwa tumepoteza maisha ya mtu, ukipangiwa zamu zingatia.

“Humu ndani (jengo) kuna ‘electronic sign’, unapaswa kusaini unapoingia na kutoka, siku tukifanya ‘analysis’, tutajua tu kwa sababu itasoma iwapo ulikuwepo au hukuwepo kazini,” alisema.

Alisema daktari huyo alichukuliwa hatua wiki mbili zilizopita (Desemba 29, mwaka huu) baada ya uchunguzi kubaini alikuwa ametenda kosa.

“Usipokee rushwa, na juzi walikuja hapa watumishi wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), natumaini wamewaeleza kwa kina, pia zingatieni kuvaa mavazi ya staha,” alisema.

Akifafanua sakata hilo, Mkuu wa Idara ya Rasilimali Watu wa Taasisi hiyo, Ghati Chacha, alisema daktari huyo alibainika kusafiri nje ya nchi bila kibali.

“Hakuwepo kazini, alikuwa mtoro, kamati ya nidhamu ilikaa na kufuatilia hadi Idara ya Uhamiaji na uchunguzi ikabainika kweli alitenda kosa, tulipatiwa taarifa pale uhamiaji na ilionyesha katika siku ambazo hakuwepo, alikuwa amesafiri kwenda Addis Ababa na hakuwa ameomba kibali kama ambavyo inatakiwa,” alisema.

Kuhusu ajira hizo mpya, alisema JKCI walipatiwa kibali na Serikali kuajiri watumishi 57 na kwamba walijitokeza waomba kazi 56 na nafasi moja bado haijajazwa.

“Watumishi 52 ndio ambao wameripoti hadi sasa, kati yao 23 ni wanaume na 29 wanawake, nafasi moja ambayo ni ya ofisa mipango bado ipo wazi,” alisema.

Mwisho

 

Hali ya mapacha walioungana yaimarika

 

Na VERONICA ROMWALD – DAR ES SALAAM

HALI ya kiafya ya mapacha, Maria Mwakikuti na Consolata Mwakikuti

imeimarika baada ya kupatiwa matibabu ya awali katika Taasisi ya Moyo

Jakaya Kikwete (JKCI) walikolazwa kwa matibabu ya moyo.

Akizungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam jana, Mkurugenzi Mtendaji wa JKCI, Profesa Mohamed Janabi, alisema bado wanaendelea kuwafanyia uchunguzi.

“Wanaendelea vizuri si kama walivyoletwa awali juzi tulipowapokea, bado tunawafanyia vipimo na jopo la madaktari bingwa naliongoza mimi mwenyewe.

“Kwa msingi huo, naomba ndugu waandishi wa habari mtupe muda ili tukamilishe uchunguzi tunaofanya kisha tutatoa taarifa kamili juu ya kile tulichokibaini,” alisema.

Profesa Janabi alisema ikiwa watoto hao watakutwa na tatizo la moyo pekee, wanao uwezo wa kuwatibu.

“Japo wamefikishwa hapa kwa tatizo la moyo, lakini ikibidi tutahusisha pia madaktari bingwa wengine wa Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) na hata Taasisi ya Tiba ya Mifupa, Ubongo, Uti wa Mgongo na Mishipa ya Fahamu Muhimbili (MOI) katika matibabu yao,” alisema.

Mapacha hao, walioungana kuanzia sehemu ya kifua, walifikishwa usiku wa juzi katika taasisi hiyo wakitokea mkoani Iringa baada ya kuugua.

Juzi, akizungumza na MTANZANIA, mlezi wa watoto hao, Fransisca Mlangwa, alisema walianza kuugua tangu Desemba 27, mwaka jana.

Alisema Consolata ndiye ambaye alikuwa na hali mbaya zaidi ya Maria, ikabidi wawapeleke katika Hospitali ya Iringa.

“Walikuwa wanatapika na kukohoa, ikabidi tuwawahishe hospitalini, wakahudumiwa, lakini haemoglobin yao ikawa ndogo, wakaongezewa damu na kupatiwa matibabu mengine,” alisema.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles