30.2 C
Dar es Salaam
Saturday, April 20, 2024

Contact us: [email protected]

Daktari bingwa atoa somo kwa wagonjwa wa macho

AVELINE KITOMARY – DAR ES SALAAM

DAKTARI  Bingwa wa Magonjwa ya Macho kutoka Hospitali ya CCBRT, Cyprian Ntomoka, amewaonya watu wanaotoa elimu  zenye upotoshaji kuhusu matibabu ya macho na kusababisha madhara kwa jamii.

Akizungumza na MTANZANIA jana hospitalini hapo alisema jambo hilo limekuwa changamoto kwao kutokana na baadhi ya watu kushindwa kuamini tiba wanazopewa ikiwamo za miwani.

“Changamoto iliyoko kwenye mfumo wa afya ni kwamba sasa kuna waalimu wengi wanaohusiana na afya kwenye tiba mbadala, watu wanaohusika wamekuwa na maoni mengi  kuhusiana na afya  na viungo vya mwili kwa ujumla.

“Sitaki kusema sana elimu ya hawa watu wa tiba mbadala ikoje kuhusiana na mwili na utendaji wa mwili, lakini ukweli ni kwamba unakuta mtu anaongea kuhusu mfumo fulani wa utendaji wa mwili ukajiuliza hivi mimi na yeye nani kaenda darasani, utakuta anaongea vitu ambavyo havipo,”alisema Dk Ntomoka .

Alisema matibabu ya macho yanahitaji vipimo ili kugundua aina ya matibabu ambayo mgonjwa anastahili hivyo ni vyema jamii kuwasikiliza madaktari zaidi.

“Kuna mmoja ambaye alishawahi kuwaambia watu anaweza kutibu mtoto wa jicho bila kufanya upasiako, kwa elimu yangu kama daktari sijawahi kuona mahali popote duniani  mtu mwenye mtoto wa jicho akapona bila kufanyiwa upasiaji.

Akielezea umuhimu wa lishe, alisema ni sehemu muhimu ya kuboresha uoni na sio tiba ya uoni kama baadhi ya watu wanavyodai.

“Elimu rasmi ya afya inatambua umuhimu wa lishe katika kuhakikisha mfumo wa mwili unafanyakazi kwasababu chakula ndio kinafanya mfumo wa mwili kufanya utendaji kazi wake.

Mfano kwenye jicho kuna kitu kinaitwa vision pigment ambazo hufanya jicho lifanye kazi yake ya kuona, hizi hujengwa kwa vitamin A lakini hii inafanyika kwa mtu ambaye seli zake ni nzima, lakini seli zikishapata matatizo inahitaji matibabu na sio kula chakula.

“Ninamashaka ya mtu kushauriwa kula karoti, matango, mboga za majani lakini ukweli ni kwamba hizo haziwezi kumsaidia, anatakiwa kutibiwa sababu za kutokuona halafu akishapona akale hizo mbogamboga, unaweza kuongeza kiasi cha uone baada ya kugundua tatizo, kutibiwa na kuboresha kile ambacho umepata kwenye matibabu,”alieleaza.

Dk Ntomoka alisema matatizo ya macho ya kutokuona  mbali au karibu ni suala la maumbile ambapo moja nya tiba ni kuvaa miwiwani ili uweze kuona mbali au karibu.

Aliwashauri watu kutafuta  madaktari ili  kujua tatizo la macho yao waweze kujua wanahitaji aina gani ya matibabu.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles