25.2 C
Dar es Salaam
Friday, April 19, 2024

Contact us: [email protected]

DAKTARI AFICHUA ONGEZEKO LA WATOTO WANAOZALIWA NA JINSIA MBILI

  • Asema yupo mvulana wa miaka 29 ambaye amekuja kujulikana ana mfumo wa uzazi wa mwanamke

NA VERONICA ROMWALD – DAR ES SALAAM


DAKTARI Bingwa wa Upasuaji wa Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH), Zaitun Bokhari amesema tatizo la watoto wanaozaliwa na jinsia tata linaonekana kuongezeka nchini.

Dk. Bokhari alisema hayo juzi katika mahojiano maalum na MTANZANIA Jumamosi kuhusu tatizo hilo liitwalo kitaalamu Ambiguous Genitalia, ikiwa ni neno linalotumika kuelezea viungo vya siri vya mtoto aliyezaliwa ambavyo ni vigumu kujua kama ni wa kike au kiume.

“Yaani unakuta mtoto wa kike amezaliwa huku kinena chake kinakuwa kikubwa kuliko kawaida ambacho mtu huweza kukifananisha kama uume wa mtoto ambaye amezaliwa.

“Lakini anakuwa na mashavu ya uke kama kawaida pamoja na yale matundu mengine muhimu kwenye uke wake, wakati mwingine unakuta yale mashavu yameungana, ila kile kinena kinakuwa kidogo na kule chini unakuta kuna njia ya mkojo, ni maumbile yanayoleta utata,” alisema.

Alisema kutokana na mkanganyiko na wazazi wengi kutokuwa na uelewa wa kutosha hushindwa kutambua mapema na kudhani ni hali ya kawaida kumbe la!.

“Unakuta mtoto analelewa kama vile wa kiume kumbe ni wa kike au analelewa kama wa kike kumbe ni wa kiume,” alisema.

Alisema kwa kuwa Muhimbili ni Hospitali inayotoa matibabu ya kibingwa hupokea wagonjwa kutoka mikoa yote hata hivyo wengi hufikishwa wakiwa wamechelewa.

“Hii ni changamoto tunayoiona, bado wazazi wengi hawana uelewa kulitambua.

“Tunapokea watoto wenye umri wa miaka mitatu, saba, nane na hivi karibuni tumepokea kijana mwenye miaka 29, ambaye amelelewa kama mtoto wa kiume maisha yake yote, tayari ana mpenzi wake lakini hadi alikuja hospitalini baada ya kujiona anapatwa na hali tofauti na maumbile yake.

“Hupata hedhi kama mwanamke, tulipomchunguza tuliona ana kinena na uke na tulifanya uchunguzi kwa vipimo vya kitaalamu zaidi vikatuonesha ndani ya mwili wake ana mfumo wa uzazi wa mwanamke.

“Ana uterasi (tumbo la uzazi), mirija yote miwili na vifuko vya mayai anavyo na tuliona kuna yai lilikuwa limeshapevuka tayari kupata hedhi,” alibainisha.

Aliongeza “Hii ni changamoto iliyopo ambayo jamii inapitia, kuna mtoto mwingine tulimpokea hapa ana miaka 14, kaanza kuota maziwa sasa wazazi wake wamempeleka shule ya bweni.

“Kule mwalimu mkuu alishtuka baada ya kuona mtoto huyo ameona hedhi, akachukua hatua kumleta tumchunguze, hivi sasa tunasubiri vipimo vya (DNA) kutoka Ofisi ya Mkemia Mkuu wa Serikali kwa sababu kwa hicho tunaweza kutoa maamuzi, inakuwa ni ‘official document’,” alisema.

Alisema njia rahisi mama kumtambua mtoto ni kulinganisha maumbile ya mtoto wake na ya kwake ikiwa ni wa kike au ya baba wa mtoto ikiwa ni wa kiume.

Wakati Dk. Bokhari akieleza hayo, juzi akizungumza katika mdahalo maalum kuhusu namna ya kutambua tatizo hilo na madaktari bingwa wa MNH, Profesa Sten Drop wa nchini Netherlands alisema kwa kawaida jinsia ya mtoto hutegemea mbegu ya baba kama imebeba vinasaba vya kike au vya kiume.

“Jinsia ya mtu hutokea mara baada ya mimba kutungwa. Hata hivyo viungo vya ndani na vya nje vya uzazi vinategemea homoni ambazo zimebebwa kwenye vinasaba,” alisema.

Alisema hitilafu yoyote ambayo husababisha homoni hizo zisifanye kazi vizuri mtoto akiwa tumboni huweza kusababisha kutotengenezwa kwa viungo vya jinsia husika au hata kutengenezwa kwa jinsia zote mbili.

Katika mahojiana yake na gazeti hili Dk. Bokhari alisema pamoja na kwamba hadi sasa bado wataalamu hawajajua kinachosababisha hitilafu hizo.

“Ila kuna visababishi vinaweza kufanya mtoto kuzaliwa na tatizo hili, visababishi hivyo hasa humpata mama kwa mfano magonjwa mbalimbali, ukosefu wa virutubishi na vinginevyo, kiujumla pia afya ya mama inaweza kuchangia kupata mtoto mwenye jinsia tata,” alisema.

Alisema kwa mwezi hospitalini hapo hupokea kati ya watoto watano hadi sita wanaokabiliwa na tatizo hilo.

“Yaani unakuta mtoto wa kike amezaliwa huku kinena chake kinakuwa kikubwa kuliko kawaida ambacho mtu huweza kukifananisha kama uume wa mtoto ambaye amezaliwa.

“Lakini anakuwa na mashavu ya uke kama kawaida pamoja na yale matundu mengine muhimu kwenye uke wake, wakati mwingine unakuta yale mashavu yameungana, ila kile kinena kinakuwa kidogo na kule chini unakuta kuna njia ya mkojo, ni maumbile yanayoleta utata,” alisema.

Dk. Bokhari alisema Muhimbili ni Hospitali inayotoa matibabu ya kibingwa na hupokea wagonjwa kutoka mikoa yote licha ya wengi kufikishwa wakiwa wamechelewa.

TIBA IPO?

Akizungumza katika mdahalo huo maalum kuhusu namna ya kutambua tatizo hilo, Profesa Sten Drop alisema tatizo hilo ni la kidunia hata hivyo hali ni tofauti na hapa nchini.

“Katika nchi nyingine watoto wa namna hii hutambulika punde tu baada ya kuzaliwa na hivyo mchakato wa maamuzi huanza kufanyika,” alisema.

Alisema tatizo hilo hutibika hata hivyo muhusika hulazimika kufanya uamuzi mgumu.

“Sheria ipo inaturuhusu lakini lazima na muhusika akubali kufanyiwa upasuaji huo hasa kwa wale ambao tayari wana umri wa miaka 18 na kuendelea,” alisema.

Alisema hata hivyo wengi hushindwa kufanya maamuzi kwa kuhofia unyanyapaa watakaofanyiwa kwenye jamii pale itakapogundulika kuwa walizaliwa na jinsia tata.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles