24.2 C
Dar es Salaam
Thursday, April 25, 2024

Contact us: [email protected]

Clinton ‘ashinda’ mdahalo wa kwanza

671024373jh00050-hillary-cl

NEW YORK, MAREKANI

UCHUNGUZI wa maoni ya umma nchini Marekani unaashiria mgombea wa kiti cha urais wa Marekani kupitia Chama cha Democrat, Hillary Clinton, amemshinda mpinzani wake, Donald Trump katika mdahalo wa kwanza uliofanyika usiku wa kuamkia jana.

Moja ya chunguzi hizo ni ule wa haraka uliofanywa na televisheni ya CNN kwa kuwashirikisha wapiga kura 521, ambapo asilimia 62 walisema Clinton alishinda mdahalo huo dhidi ya asilimia 27 ya Trump.

Hata hivyo, tafiti nyingine zilizoendeshwa na mitandao yenye mwelekeo wa kumuunga mkono Trump kama vile Fox  ilimpatia bilionea huyo ushindi wa asilimia 61.3 dhidi ya 33.7 za Clinton.

Awali Trump na Clinton walisalimiana kwa kupeana mikono na kutabasamu kabla ya kuanza mdahalo huo wa kwanza kati ya mitatu ya urais, ambao umekuja wakati kinyang’anyiro cha kuelekea Ikulu kikianza kuwa kikali.

Mdahalo huo uliojaa mivutano na kuonyeshwa moja kwa moja katika televisheni na kushuhudiwa na watazamaji zaidi ya milioni 100, uliwapambanisha kuhusu ajenda zao, ambapo kila mmoja alimshambulia mwenzake.

Ukiwa umesubiriwa kwa hamu na kufanyika katika Chuo Kikuu cha Hofstra mjini hapa, mdahalo huo uliangazia sera za kiuchumi za wagombea hao, mahusiano ya jamii, vita dhidi ya kundi linalojiita Dola la Kiislamu (IS), uhalifu na sera ya kigeni ya Marekani.

Clinton alisema alichopendekeza kuhusu kodi ni kuongeza kiasi cha malipo kwa matajiri kwasababu wao wamepata faida katika uchumi, na ni wakati mwafaka kwao kulipa zaidi ili kusaidia nchi.

Lakini Trump alimshambulia Clinton juu ya sera zake akisema ‘ni maafa’ na kuwa mpango wake wa kupunguza kodi kwa matajiri utatengeneza nafasi nyingi za kazi.

Wagombea hao pia walijadili kitisho cha ugaidi wakijikita zaidi na kundi linalojiita Dola la Kiislamu (IS) nchini Syria a Irak.

Trump anayegombea kupitia chama cha Republican alionekana mwenye ujasiri mwanzoni wakati akionyesha upinzani wake kwa mikataba ya kibiashara, akieleza maoni yake kuhusu uhusiano wa jamii na kupambana na uhalifu.

Lakini wakati mdahalo ulipogeukia sera ya kigeni, Clinton alitawala jukwaa na kumwendesha puta Trump licha ya juhudi zake za mara kwa mara za kuingilia kati.

Aidha katika mdahalo huo, kila mgombea alijaribu kumweleza mwenzake kuwa asiyefaa kuongoza Marekani.

Katika hilo walilumbana kuhusu masuala kadhaa tata kuanzia uamuzi wa Trump kutotangaza taarifa ya mapato na matumizi hadi uamuzi wa Clinton kutumia anuani ya binafsi ya barua pepe wakati akiwa waziri wa mambo ya nje na kitendo cha Trump kueneza uongo kuwa Rais Barack Obama hakuzaliwa Marekani.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles