23.7 C
Dar es Salaam
Friday, April 19, 2024

Contact us: [email protected]

Chura ya Snura bado kimbembe

SNURA JUKWAANI

NA FESTO POLEA,ZANZIBAR

LICHA ya kufungiwa na mamlaka husika za serikali kutokana na video yake kukiuka maadili ya Mtanzania, wimbo wa ‘Chura’ ulioimbwa na Snura Mushi ‘Snura Majanga’ unaonekana kumpa changamoto kwa mashabiki wake kila wanapomtaka auimbe.

Katika kila onyesho lake mjini hapa, mkali huyo anayetamba kwa sasa na wimbo mpya wa ‘Shindwe’ unaomaanisha kishindo, mashabiki wamekuwa wakimshinikiza aimbe wimbo huo.

SNURA NA MAPAPARAZI

Katika mkutano na waandishi wa habari, wasanii wa muziki, filamu pamoja na wadau wa sanaa kwa jumla liliibuka swali likimtaka Snura atoe ladha ya wimbo wake mpya wa ‘Shindwe’ na ule wa Chura lakini kabla ya kuimba alihoji mara mbilimbili.

Niimbe na kuonyesha Chura?” aliuliza Snura mbele ya waandishi wa habari.

Kauli hiyo iliibua pande mbili waliotaka aimbe na kumcheza Chura na wengine walipinga wakimtaka akaonyeshe usiku wakati wa shoo yake, hivyo akaimba sauti na mashairi ya wimbo wa ‘Chura’ na ‘Shindwe’ bila kucheza.

DJ SAMIRA KUTOKA MAREKANI

Kabla ya Snura kufungua pazia la watumbuizaji katika usiku huo wa Bi Kidude katika Tamasha la 19 la Kimataifa la Filamu za Nchi za Jahazi linalofanyika visiwani Zanzibar katika viwanja vya Ngome Kongwe, Dj Samira kutoka Marekani alionyesha uwezo wake wa kutumia mashine kwa kuchanganya nyimbo za wasanii mbalimbali wa nje.

Uwezo wa Dj huyo ulivuta watu wengi katika ukumbi huo na baada ya kumaliza sauti za shangwe zilisikika zikiita ‘Chura, chura churaa’.

SHOO YA SNURA

Mwongoza shoo hiyo aliwahoji mashabiki nani wa kuanza kufanya shoo kati ya watumbuizaji wawili pekee waliopata nafasi ya kutumbuiza usiku huo wa Bi Kidude akiwepo Baby J na Snura Majanga na mashabiki wakataka Snura aanze kisha Baby J amalize.

Snura alipopanda shangwe zililipuka tena kwa kuimba: “Churaaa, churaaa, churaaa, tunataka churaaa,” lakini Snura akaweza kucheza na akili za mashabiki wake, akaanza na wimbo wa Majanga huku akitumia vyema mwili wake na wanenguaji wake kuwapoteza mashabiki baada ya kufurahia wanavyofanya jukwaani.

Lakini licha ya mashabiki hao kufurahia nyimbo hizo ukiwemo wimbo wake mpya wa ‘Shindwe’ bado hakukwepa changamoto ya kutakiwa kuimba wimbo wa Chura kwani kelele za shangwe zikimtaka aimbe wimbo huo zilisikika upya ukumbi mzima.

Mashabiki: Tunataka uimbe Chura, imba chura, tunataka Churaaaaa!

Snura: Nini mbona siwaelewi?

Mashabiki: Churaaaaaa!

Snura: Mnataka niimbe Chura kwani hamjayaona mapichapicha yake? Sawa… Dj kabla hujaanza ngoja kwanza niwaonyeshe hawa watoto (wanenguaji wake) wanadai wamenifunika haya lete mambo.

ANAMALIZA SHOO

Shoo ya Snura inamalizika kwa kunengua midundo (bit) ya wimbo wa Chura huku wakionyesha staili mbalimbali zinavyotakiwa kuchezwa katika biti hiyo, jambo ambalo liliwafurahisha mashabiki hao hadi mwisho wa shoo hiyo.

Baada ya shoo hiyo, Swaggaz lilifanya mahojiano naye kuhusiana na changamoto anazopata anapotakiwa kuimba wimbo huo, akiwa jukwaani na walipofikia na mamlaka zilizofungia video ya wimbo wake huo.

“Ni changamoto kwa kweli kila ninapopanda jukwaani licha ya kuimba nyimbo nyingine na kufurahiwa sana lakini lazima wapige kelele niimbe wimbo wa Chura, unanipa changamoto kubwa kwa kuwa umefungiwa na bado sijapewa ruksa ya kurudia video yake.

“Mara ya kwanza ulipofungiwa nilitakiwa nibadilishe script ya video ya wimbo huo, nikabadilisha lakini nilipowapelekea waliikataa wakanitaka nibadilishe tena wakidai itafanana na ile. Nimeandika tena script mpya na nimeshawapelekea wahusika lakini bado sijajibiwa,’’ anaeleza Snura.

Hata hivyo Tamasha la Ziff kesho Jumapili, litatia nanga ambapo leo usiku filamu mbalimbali zitatunukiwa tuzo za ushindi kwa vipengele tofauti na tuzo nyingine zitatolewa kesho.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles