26.2 C
Dar es Salaam
Thursday, April 25, 2024

Contact us: [email protected]

Chanjo ya Ukimwi kujaribiwa kesho

Ofisa Mtendaji Mkuu wa Baraza la Tafiti za Kitabibu Afrika Kusini
Ofisa Mtendaji Mkuu wa Baraza la Tafiti za Kitabibu Afrika Kusini, Glenda Gray

JOHANNESBURG, AFRIKA KUSINI         

CHANJO mpya ya kupambana na virusi vya Ukimwi (VVU) itafanyiwa majaribio yatakayozinduliwa kesho nchini Afrika Kusini.

Wanasayansi wamesema chanjo hiyo inaweza kupigilia msumari katika jeneza la maradhi hayo endapo itaonyesha mafanikio.

Utafiti uitwao HVTN 702, umelenga kuwahusisha wanaume na wanawake 5,400 walio katika mazingira hatarishi zaidi wenye umri kati ya miaka 18 na 35 katika miji 15 nchini humo.

Litakuwa jaribio la chanjo la kimaabara kubwa na la kisasa zaidi kuwahi kufanyika nchini Afrika Kusini, ambako watu zaidi ya 1,000 huambukizwa VVU kila siku.

“Iwapo itaenda sambamba na silaha zetu zilizothibitishwa za kukabiliana na VVU, chanjo salama na fanisi hatimaye itapigilia msumari katika jeneza la VVU.

“Hata chanjo yenye ufanisi wa kujitosheleza inaweza kwa kiasi kikubwa kupunguza mzigo wa VVU katika nchi na makundi ya watu wenye viwango vya juu vya maambukizo kama Afrika Kusini,” alisema Anthony Fauci, ambaye ni Mkurugenzi wa Taasisi ya Taifa ya Serikali ya Marekani ya Maradhi ya Kuambukiza na Mizio (NIAID).

Chanjo inayojaribiwa katika njia ya HVTN 702, inatokana na majaribio ya mwaka 2009 nchini Thailand, ambayo ilionekana kuwa na ufanisi wa asilimia 31.2 wa kuzuia maambukizo ya VVU kwa kipindi cha miaka mitatu na nusu ya ufuatiliaji baada ya chanjo.

Chanjo hiyo mpya ambayo imelenga kutoa kinga zaidi na endelevu, imeandaliwa katika mazingira yanayoendana na aina za VVU zinazotawala nchini Afrika Kusini.

“VVU ni tishio kubwa kwa Afrika Kusini, tumeanza utafiti wa kisayansi ambao unaweza kutoa matumaini makubwa kwa nchi yetu.

“Iwapo chanjo ya VVU itaonyesha ufanisi Afrika Kusini, itaweza kwa kiasi kikubwa kubadili mwelekeo wa ugonjwa huu hatari,” alisema Glenda Gray, Ofisa Mtendaji Mkuu wa Baraza la Tafiti za Kitabibu Afrika Kusini

Watu waliojitolea kushiriki katika utafiti huo unaofadhiliwa na NIAID pamoja na mambo mengine, watachomwa sindano tano za chanjo kipindi cha mwaka mmoja.

Washiriki ambao wataambukizwa na VVU katika jamii watawasilishwa kwa watoaji huduma za afya katika maeneo yao kwa matunzo na tiba pamoja na kupokea ushauri nasaha wa namna ya kupunguza hatari za kusambaza virusi.

Afrika Kusini ina watu milioni 6.8 wanaoishi na VVU, lakini programu zake za kukabiliana na maradhi hayo zimeonyesha mafanikio.

Miongoni mwao ni usambazaji wa dawa za kupunguza makali ya maradhi hayo, ambayo kwa mujibu wa Serikali ni kubwa kuliko zote duniani.

Wastani wa umri wa kuishi ambao umeshuka kadiri janga la ugonjwa huo lilivyokuwa likikua, kwa sasa umepanda kutoka miaka 57.1 mwaka 2009 hadi 62.9 mwaka 2014.

Matokeo ya utafiti kuhusu chanjo hiyo mpya yanatarajia kutolewa mwishoni mwa mwaka 2020.

Kwa mujibu wa takwimu rasmi za mwaka juzi, mbali ya Afrika Kusini inayoongoza kwa wingi wa watu wanaoishi na VVU duniani, Afrika imetoa mataifa saba katika orodha ya vinara 10.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles