23.7 C
Dar es Salaam
Friday, April 19, 2024

Contact us: [email protected]

California yatangaza hali ya hatari virusi vya corona

CALIFORNIA, MAREKANI 

CALIFORNIA imetangaza hali ya hatari baada ya kutoa taarifa  ya kifo cha kwanza  kilichotokana na maambukizi ya virusi vya corona katika jimbo hilo na hivyo kufanya vifo vya nchi nzima ya Marekani kufikia 11.

Wakati huo huo Shirika la Fedha Duniani (IMF) limetangaza kutoa dola bilioni 50 kuzisaidia nchi zenye kipato cha chini zilizoathirika na virusi vya corona huku likitoa onyo kwamba tayari virusi hivyo vimeathiri ukuaji wa kiuchumi kwa mwaka huu ukilinganisha na mwaka jana .

Katika kisa kilichotokea California, mzee wa miaka 71, ambaye mauti yalimkuta hospitali karibu na Sacramento, maofisa wanasema alikuwa na hali mbaya ya kiafya na alikuwa kwenye meli.

Ikulu ya Marekani imeamua kutanua huduma ya kupima virusi hivyo nchi nzima.

Hadi sasa kuna wagonjwa 150 wenye virusi vya corona walioripotiwa nchini Marekani katika majimbo yake 16.

Duniani kote mamlaka zimethibitisha zaidi ya kesi 92,000 za virusi hivyo ambapo China pekee ina kesi 80,000.

Watu 3,000  wamekufa duniani kote, wengi wao wakiwa ni kutoka nchini China. 

Kati ya vifo 11 vilivyotokea nchini Marekani 10 vimetokea katika jimbo la Washington, lakini mripuko wa virusi hivyo  umefika Texas na Nebraska.

Wakati huo huo, Washington na Florida  wote wametangaza hali ya hatari mwishoni mwa wiki iliyopita kama njia ya kusaidia kuzuia maambukizi ya virusi hivyo.

KISA CHA CALFORNIA

Inaaminika kuwa mtu huyo aliyekufa California aliathirika na virusi hivyo wakati akiwa ndani ya meli ya Grand Princess, ambayo inafanya safari zake kutoka San Francisco kwenda Mexico mwezi uliopita.

Baada ya meli kutia nanga San Francisco Februari 21, maelfu ya abiria wengine walipanda na wengine waliteremka na kisha meli hiyo ikaelekea Hawaii.

Abiria takribani 62 walikuwa kwenye safari za Mexico na Hawaii na walizuiwa vyumbani mwao kwa ajili ya kuchukuliwa vipimo.

Meli yenyewe ya The Grand Princess imetia nanga katika pwani ya California, na Gavana wa jimbo hilo Gavin Newsom  amesema abiria  11 na wafanyakazi 10 wa meli hiyo wameathirika na virusi hivyo.

Mark Pace na mkewe Beth ni miongoni mwa abiria waliokuwa ndani ya meli hiyo. 

Walisema waligundua mabadiliko kadhaa ndani ya meli hiyo.

Kwamba ili waweze kuchukua sahani kwa ajili ya kwenda kufuata chakula walilazimika kuosha mikono kwa sabuni maalumu. 

Pia hawakuruhusiwa kujichotea chakula.

” Tulikuwa na shaka, tulijua kuna uwezekano wa  kuwako jambo hili. Tulikuja tukiwa tumejiandaa kwa kuchukua dawa za wiki mbili za ziada na kompyuta yangu ndogo ili niweze kufanya kazi ikiwa tutafungiwa,”  alisema Pace ambaye alikuwa ametoka kusheherekea kumbukumbu ya kuzaliwa ya mkewe katika visiwa kadhaa.

Meli hiyo inaendeshwa na Carnival, ambao meli yao nyingine ya Diamond Princess iliwekwa karantini mwezi uliopita baada ya abiria kadhaa kugundulika kuwa na virusi hivyo na kutia nanga katika Pwani ya  Japan.

Serikali ya Marekani kwa sasa imezuia raia yeyote wa kigeni aliyekuwa ametembelea China ambako virusi hivyo vilianzia mwezi Desemba kutoingia nchini humo.

Makamu wa Rais wa Marekani, Mike Pence alisema juzi kwamba Wamarekani watachukuliwa vipimo vya virusi vya corona iwapo datkari ataagiza kufanya hivyo.

Pence, ambaye anaongoza mipango ya kukabiliana na ugonjwa huo, pia alisema kuwa Ikulu ya Marekani itaanza kutoa taarifa juu ya virusi hivyo kwa njia ya camera.

Kwa kuongezea vituo vy Kuzuia na Kudhibiti magonjwa nchini Marekani vitaongeza vizuizi vilivyopo kwenye vipimo na kutoa miongozo mipya ya kuharakisha vipimo kwa wale ambao wanahofu kuwa  wameambukizwa.  

Lakini wengine wanahoji jinsi ahadi hii itakavyotekelezwa, kwani maabara za afya za umma zinasisitiza uwezo wao wa usindikaji wa vipimo una ukomo.

Lakini pia kuna maswali mengi kuhusu gharama, wakati kukiwa na ripoti za Wamarekani wasio na bima ambao wanatakiwa kulipa hadi dola 1,000 (£780) kwa kipimo hicho.

Baraza la Wawakilishi la Marekani limeidhinisha Dola bilioni 8.3 za msaada wa dharura kwa ajili ya kupambana na virusi hivyo vya corona.

Baadhi  ya maofisa wa afya wanaushutumu uongozi wa Rais Donald Trump kwa kusuasua kupambana na virusi hivyo, huku shaka ikitiliwa zaidi kwenye uhaba wa vipimo nchini kote.

HALI ILIVYO DUNIANI KOTE

Eneo ambalo limeshambuliwa zaidi na virusi hivyo  nje ya China ni Korea Kusini ambako juzi waliripoti  maambukizi mapya 516  na hivyo kufanya jumla kufikia 5,766. Vifo katika nchi hiyo vimefikia 35.

Katika juhudi za kukabiliana na mlipuko huo, Waziri Mkuu wa Korea Kusini Chung Sye-kyun ametangaza kuzuia kuingizwa nchini humo maski za kuziba uso.

Australia kwa upande wake imezuia mgeni yeyote kutoka Korea Kusini. 

Watu wawili wemekufa kwa virusi hivyo nchini Australia, na kesi nyingine 53 zimeripotiwa.

Wakati huo huo China imeripoti kesi mpya 139  na vifo 31  vyote kutoka katika jimbo la Hubei vilikoanzia virusi hivyo.

Shule zimefungwa kwa karibu siku 10 nchini Italia.taifa hilo nalo limeshambuliwa na virusi hivyo.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles