24.2 C
Dar es Salaam
Thursday, April 25, 2024

Contact us: [email protected]

Bolt yabisha hodi Arusha, Zanzibar

Mwandishi wetu

Kampuni inayokua kwa kasi katika utoaji wa huduma za usafiri kwa njia ya mtandaoni barani Ulaya na Afrika- BOLT, inatarajia kuzindua huduma zake katika miji mikubwa miwili nchini Tanzania ikiwa ni hatua mojawapo ya kuendelea kupanua huduma za usafiri katika soko lake la ndani ya nchi.

Akizungumza na waandishi wa habari jana Septemba 4, 2019 jijini Arusha, Meneja Mkazi wa Bolt Tanzania Remmy Eseka alisema huduma hiyo pia itaanza kupatikana wiki ijayo Visiwani Zanzibar.

Alisema uzinduzi huo wa Bolt katika jiji la Arusha na Visiwani Zanzibar unaongeza idadi ya miji ya Kitanzania inayohudumiwa na kampuni hiyo kutoka mikoa mitatu hadi mitano, na kuifanya Bolt kuwa mtoaji huduma mkubwa wa usafiri kwa njia ya mtandao katika ukanda huu wa Afrika.

 Alisema kuwa dhamira ya Bolt ni kufanya usafirishaji wa mijini kuwa rahisi zaidi na wa bei nafuu kwa watu wote na hivyo kufikia malengo ya kampuni katika utoaji huduma za usafiri na ajira ikiwa ni moja ya mchango Bolt kwa jamii.

“Baada ya miji ya Dar es Salaam, Mwanza na Dodoma kama ilivyo ada Bolt imeendelea kukua kwa kasi nchini kote. Sasa tunakusudia kujenga jamii mpya Arusha na Zanzibar kutokana na uaminifu tunaoendelea kuupata kwa Watanzania,” alisema Eseka.

“Huduma hiyo ni rahisi kutumia kwani abiria wanatakiwa kupakua programu ya Bolt kutoka kwenye maduka ya programu ya iOS au ya Android na kujaza wasifu wa mtumiaji. Wakati wapo tayari kusafiri, watumiaji hufungua program na kuweka eneo lao walilopo na mahali walipokusudia kufika.

” Programu itatoa makisio ya gharama kwa safari hiyo. Mara baada ya abiria kuomba safari, programu humwonesha madereva wa karibu ambao wanakubali safari hiyo.

“Mara tu dereva anapokubali safari hiyo, abiria wataweza kuona jina la dereva wao, picha, muundo wa gari na usajili, na kuweza kufuatilia dereva anayewafuata kwa wakati muafaka na wa kweli  lakini pia program hiyo hufanya iwe rahisi kuwa na uhakika kuwa wanaingia salama kwenye gari sahihi na dereva sahihi. Abiria pia wanaweza kutoa maelezo ya safari yao kwa kutumia program ‘ETA’ iliyomo katika kipengele cha ziada kwenye suala la usalama” alisema.

Aidha, alisema wakati safari imekamilika, malipo hufanywa na pesa taslimu, au kupitia kadi ya deni ya mpandaji aliyejiunga kwenye program hiyo. Abiria na madereva wanaweza kupima kila mmoja kati ya nyota tano na kutoa maoni kuhusu umahiri wa utumiaji programu ya Bolt.

Pia Bolt tayari imewasajili madereva katika miji ya Arusha na Visiwani Zanzibar, ambao wote wanapokea asilimia 80 ya nauli zote zinazolipwa na abiria. Hata hivyo madereva wanaotumia Bolt wanaweza kuchagua masaa mangapi wanaendesha na wanaweza kufanya kazi katika maeneo yoyote wanayotaka.

“Magari ya Madereva lazima yawe yamesajiliwa kuanzia mwaka 2000 au mapya zaidi. Gari lazima iwe na milango minne (Toyota Corolla, aina ya Hyundai, Kia Rio, nk). Hii inamaanisha kuwa kila mtu akipanda safari kupitia Bolt anaweza kuwa na hakika kwamba watafika salama kwao na kwa raha,” alisema.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles