30.2 C
Dar es Salaam
Thursday, March 28, 2024

Contact us: [email protected]

Bilal aongoza mamia kumuaga Mchungaji Mtikila

LTUNU NASSOR NA KOKU DAVID, DAR ES SALAAM

MAKAMU wa Rais, Dk. Mohamed Gharib Bilal, jana ameongoza mamia ya wakazi wa Jiji la Dar es Salaam kuaga mwili wa aliyekuwa Mwenyekiti wa Chama cha Democratic (DP), marehemu Mchungaji Christopher Mtikila.

Akizungumza baada ya jeneza la mwili wa Mchungaji Mtikila kuwasili kwenye Ukumbi wa Karimjee, Dk. Bilal alisema Mchungaji Mtikila alikuwa mtu jasiri na aliyependa kushirikiana na wenzake na kuheshimu mawazo ya wengine.

Alisema mchango wake, ulionyesha uhuru kwa jamii iliyokuwa na mawazo tofauti kuendelea kusikika pamoja na kuwa mtetezi wa watu.

“Alikuwa anatetea haki kwa nguvu zake zote, jambo ambalo Watanzania wote tunatakiwa kuwa hivyo, tutakumbuka mema aliyoyafanya katika taifa letu,” alisema Dk. Bilal.

Rais Jakaya Kikwete, alifika ukumbini na kusaini kitabu cha maombolezo, kisha akaondoka.

Akizungumza kwa niaba ya Serikali, Msajili wa Vyama vya Siasa, Jaji Francis Mutungi, alisema Mchungaji Mtikila alikuwa mtu wa kupenda na kufuata sheria.

Alisema siku zote alikwenda mahakamani bila ya kuandamana pale alipoona haki haikutendeka.

Jaji Mutungi alisema kuwa Mchungaji Mtikila alikuwa mpambanaji asiyekata tama, na kiongozi mwenye msimamo mkali  uliosababisha kipengele namba 12 cha sheria kilichokuwa kinazua maandamano kuondolewa.

“Hata kama hakupata haki yake, alikwenda kuifuata mahakamani, alikuwa akivuka mipaka hadi mahakama za Afrika Mashariki na Afrika ili kupata mwongozo,” alisema Jaji Mutungi.

Naye mdogo wa marehemu, Maria Mtikila, alisema kaka yake alikuwa kama mshumaa uliowaka, sasa umezimika.

Alisema hawaoni mtu anayeweza kuvaa viatu vyake kutokana na ujasiri aliokuwa nao kutetea haki za wanyonge na kufuata sheria.

Naye Makamu wa Kwanza wa Rais wa Serikali ya Umoja wa Kitaifa Zanzibar (SUKI), Maalim Seif Sharif Hamad, alisema alimfahamu Mchungaji Mtikila wakati wakiwa katika harakati za siasa, hasa kutokana na uwazi aliokuwa nao wa kutokuficha maoni yake aliyoamini.

Alisema Mchungaji Mtikila alikuwa akisimamia jambo aliloliamini mwanzo hadi mwisho, kitendo kilichofanya nchi isimame katika misingi bora.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Baraza la Vyama vya Siasa Tanzania, Peter Mzirai, alisema Mchungaji Mtikila alikuwa miongoni mwa wapambanaji waliofanikisha kupitishwa mgombea binafsi.

“Watu hawamfahamu vizuri Mchungaji Mtikila, alikuwa  mpole sana, mpiganaji na mwenye kupenda kufuata sheria,” alisema Mzirai.

 

JENEZA LAKE

Katika hatua nyingine, jeneza lililobeba mwili wa Mchungaji Mtikila, liliwasili kwenye ukumbi wa Karimjee, likiwa limefunikwa bendera ya Tanganyika.

Itakumbukwa wakati wa uhai wake, marehemu Mchungaji Mtikila siku zote alikuwa anapigania kuwapo kwa Serikali ya Tanganyika.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles