24.2 C
Dar es Salaam
Tuesday, April 16, 2024

Contact us: [email protected]

BEI YA NG’OMBE, MBUZI YAPANDA DAR

HALIMA ALLY(TUDARCO) Na TUNU NASSOR – DAR ES SALAAM


BEI ya ng’ombe na mbuzi   Dar es Salaam imepanda hasa katika kipindi hiki cha Sikukuu ya Eid El-Hajj ambayo itaswaliwa kesho nchini.

MTANZANIA ilifanya uchunguzi ambao katika soko la mifugo la Pugu, ng’ombe aliyekuwa akiuzwa kwa Sh 600,000 amepanda na kufikia hadi Sh milioni 1.2 huku mbuzi kutoka Sh 120,000 hadi Sh 200,000.

Kupanda kwa bei hizo kunatokana na uzito wa Sikukuu ya Eid ya kuchinja ambako Waislamu wengi huchinja kwa lengo la kutimiza moja ya nguzo za Uislamu.

Katika eneo la Vingunguti ambako huuzwa mbuzi kwa wingi mifugo hao wanauzwa kati ya Sh 175,000 hadi Sh 200,000.

Mmoja wa wafanyabiashara katika eneo hilo, Khasimu Said alisema bei hiyo imepanda kutokana na mahitaji ya mbuzi kuwa makubwa huku wafugaji wakiuza mifugo kidogo.

“Bei zimepanda kwa sababu wakulima wamepata chakula cha kutosha hivyo hawana mahitaji wa kuuza zaidi mifugo yao,” alisema Said.

Naye muuza nyama  katika eneo la Shekilango, Chacha Mwita,  alisema bei ya nyama imeongezeka kutokana na uhaba wa ng’ombe katika kipindi cha Sikukuu ya Eid.

“Bei ya nyama kwa rejareja imepanda kutoka Sh 6,000 hadi Sh 6,500 kwa kilo kwa sababu machinjioni watatuuzia Sh 6,000 kwa kilo moja,” alisema Mwita.

Mfanyabiashara wa kuku wa Shekilango, Hassan Mussa alisema kwa sasa kuku wa kisasa wa mayai wamepanda kutoka Sh 10,000 hadi  Sh 12,000 huku wale wa nyama wakiongezeka kwa Sh 500 na kufikia Sh 6,500.

“Kuku wamepanda kutokana na kupanda kwa bei na upatikanaji mdogo wa vyakula vyake na pia vifaranga vimepanda bei,” alisema Mussa.

Meneja wa Soko la Ilala, Selemani Mfinanga, alisema katika soko hilo bei ya nyama imeongezeka kwa Sh 500 kwa kilo moja na huenda ikaongezeka zaidi kuanzia leo kutokana na maandalizi ya Sikukuu ya Eid.

“Tunatarajia kuongezeka zaidi kwa bei ya nyama ndani ya siku mbili hizi kutokana na maandalizi ya Sikukuu ya Eid,” alisema Mfinanga.

Alisema hata hivyo katika soko hilo kuku wa kienyeji pia wamepanda bei kutoka Sh 18,000 hadi kufikia Sh 20,000 na Sh 25,000.

“Nyanya zimeshuka kutoka Sh 50,000 kwa kasha moja hadi kufikia Sh 25,000 huku zilizolala zikiuzwa kwa Sh 18,000,” alisema Mfinanga.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles