23.2 C
Dar es Salaam
Friday, April 19, 2024

Contact us: [email protected]

Barua zafichua baba wa Obama alivyoteseka

Barack-Obama-Sr.NEW YORK, MAREKANI

BARUA zilizoandikwa na Barack Hussein Obama Sr. – baba wa Rais wa Marekani, Barack Obama zimefichua kuwa alikabiliana na hali ngumu ya maisha alipokuwa masomoni nchini hapa.

Barua nane zilizowekwa mtandaoni na gazeti la New York Times zinaonyesha jinsi baba huyo ambaye sasa ni marehemu, alivyokuwa akitegemea ufadhili wa wahisani kukidhi mahitaji yake muhimu akiwa nchini humo, kati ya mwaka 1958 na 1964.

Rais Obama alikuwa amezaliwa wakati baba yake akiomba baadhi ya misaada hiyo. Rekodi zinaonyesha alizaliwa Agosti 4, 1961 katika Jimbo la Hawaii.

Katika moja ya barua hizo, Obama Sr. alieleza mshangao wake jinsi gharama za maisha zilivyokuwa juu jijini Boston, ambako hakuamini hata mkate wa ‘hamburger’ uliuzwa kwa senti tano za Marekani (karibu sawa na shilingi 100 za Tanzania).

“Kufikia sasa fedha zangu zimekuwa zikiisha haraka kwa sababu nimelazimika kununua mavazi ya kukabili baridi. Kodi ya nyumba pia ni ya juu mno.

“Kiwango cha chini zaidi ambacho kinaweza kukidhi mahitaji ya mtu hapa ni dola 200 (Sh 440,000). Sina yeyote wa kumtegemea zaidi yako,” aliandika katika barua hiyo kwenda kwa Robert Sherman, Novemba 28, 1962 kuomba apatiwe dola 1,000 (Sh milioni 2.2).

Kulingana na anuani iliyoandikwa, Sherman alikuwa Mkurugenzi wa Mpango wa Misaada kwa Wanafunzi wa Shirika la Phelps Stokes Fund lililokuwa na makao makuu New York.

Ripoti ya New York Times ilisema Rais Obama alikuwa amefahamishwa kuhusu barua hizo wakati kituo cha Schomburg kilipozipata mwaka 2013, ingawa hawakusikia kauli yoyote kutoka kwake.

Hata hivyo, ofisa mmoja mwandamizi katika Ikulu ya Marekani, alisema Rais Obama amepanga kusoma barua hizo baada ya kuondoka madarakani mwaka ujao.

Katika barua nyingine iliyoandikwa kwenda kwa Sherman Juni 13, 1962, Obama Sr. aliomba nauli kutoka Hawaii kwenda Chuo Kikuu cha Harvard ambako alikuwa amefadhiliwa kusomea shahada ya uzamivu.

“Ninakuandikia barua wakati huu kwa sababu ninataabika na sina nauli. Nisipopata usaidizi nitakwama hapa,” alisema na kuongeza kwamba nauli aliyohitaji ilikuwa dola 400 (Sh 880,000).

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles