27.9 C
Dar es Salaam
Thursday, March 28, 2024

Contact us: [email protected]

Baraza la Maadili kumweka kikaangoni Ngeleja

willium NgelejaAziza Masoud na Patricia Kimelemeta, Dar es Salaam
BARAZA la Maadili ya Utumishi wa Umma jana liliahirisha shughuli za kumhoji Mkurugenzi wa Sheria wa Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Rugonzibwa Mujunangoma, baada ya eneo la mahojiano, Ukumbi wa Karimjee kutumika kwa shughuli za kuaga mwili wa aliyekuwa Mbunge wa Mbinga Magharibi, Kapteni John Komba.
Kutokana na hali hiyo, baraza hilo litaendelea na shughuli zake leo ambapo Mujunangoma atahojiwa kutokana na tuhuma za kupokea fedha za akaunti ya Tegeta Escrow.
Akizungumza na waandishi wa habari jana, Mwenyekiti wa baraza hilo, Jaji mstaafu Hamisi Msumi, alisema kutokana na kuwapo kwa dharura hiyo, hawakuweza kuendelea na shughuli za baraza kwa siku ya jana.
“Waafrika tuna utamaduni wa kuruhusu shughuli za dharura kuendelea kama hii iliyotokea ya kifo cha Kapteni John Komba ambapo shughuli za kuaga mwili wake zitafanyika katika ukumbi huu,” alisema Jaji Msumi.
Hata hivyo, Mujunangoma alifika katika eneo hilo akiwa na mawakili watatu ili waweze kumtetea katika shauri hilo lililotakiwa kuanza saa tatu kamili jana asubuhi.
Kwa mujibu wa ratiba ya mashauri ya baraza hilo, leo watamhoji Mbunge wa Sengerema, William Ngeleja, ambaye naye anadaiwa kupokea mgawo wa Sh milioni 40 katika akaunti hiyo.
Baraza hilo linatakiwa kuwahoji viongozi saba ambapo hadi sasa wamehojiwa wawili.
Waliohojiwa ni Mbunge wa Muleba Kusini, Profesa Anna Tibaijuka na Mbunge wa Bariadi Mashariki, Andrew Chenge, ambaye aliomba mwongozo wa shauri lake kurudishwa Mahakama Kuu ili kutafuta tafsiri ya zuio lililotolewa na mahakama hiyo kwa ajili ya kuzuia kujadili suala lolote linalohusu miamala ya Akaunti ya Escrow na wamiliki wake.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles