31.7 C
Dar es Salaam
Thursday, March 28, 2024

Contact us: [email protected]

Balozi Seif akunjua kucha Zbar

balozi-seifc2a0-ali-iddiNa Mwandishi Wetu, Zanzibar

SERIKALI ya Mapinduzi Zanzibar, imesema ipo tayari kutumia vyombo vyake vya dola kukabiliana na tishio lolote au mipango ya njama zinazokusudia kuleta vurugu wakati huu wa uchaguzi mkuu.

Makamu wa Pili wa Rais, Balozi Seif Ali Idd, ameyasema hayo jana katika mkutano wa hadhara wa uzinduzi wa kampeni za CCM zilizofanyika Kijiji cha Michamvi, Mkoa wa Kusini Unguja.

Alisema tayari kuna baadhi ya wanasiasa, wameanza kujiandaa kutumia makundi ya vijana ili kuleta fujo wakati wa uchaguzi mkuu kama mkakakti wao wa kufikia malengo yao kisiasa.

“Natahadharisha asijaribu mtu au kikundi chochote kufanya vurugu, safari hii tumejitayarisha kisawasawa…hatutakubali zitokee ghasia kama zile za Uamsho, atakayejaribu kuvuruga utulivu na amani atakiona cha mtema kuni,” alisema Balozi Seif.

Alisema ni jambo la kusikitisha kuona kampeni chafu zimeanza, ikiwamo kuchanwa picha za mgombea urais wa CCM, Dk. Ali Mohamed Shein katika visiwa vya Pemba na Unguja.

“Mabango ya picha za Dk. Shein yanabanduliwa, ukimuona mtu anachana kitu kisichosema ni sawa na kugombana na mwehu, hiyo ni dalili tosha kuwa wapinzani wa CCM wameshindwa kabla ya Oktoba 25,” alisema Balozi Seif.

Alisema SMZ imenunua meli ya kisasa, kupeleka nishati ya umeme wa gridi ya taifa Pemba kutoka Tanga hadi Pemba, ujenzi wa miundombinu ya barabara za viwango vya lami, uwanja wa ndege wa kisasa wa Abeid Amani Karume mbali na kupandisha bei ya zao la karafuu toka Sh 5,000 hadi Sh 14,000 kwa kilo.

Katika mkutano huo, Balozi Seif aliwanadi na kuwaombea kura wagombea wa nafasi za ubunge na uwakilishi wa majimbo yote ya Mkoa wa Kusini Unguja wanaowania kupitia CCM.

Naye mwanasiasa mkongwe, Sukwa Said Sukwa, akizungumza katika mkutano huo, alisema viongozi wastaafu wanaopanda kwenye majukwaa ya kampeni za CCM na kushindwa kuwaombea kura Dk. Shein na Dk. John Magufuli wanastahili kuchunguzwa na kuchukuliwa hatua za kinidhamu.

Sukwa alisema haiwezekani kiongozi mstaafu ambaye alifanyiwa kampeni na viongozi wenzake, leo ashindwe kumfanyia kampeni mgombea wa CCM.

 

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles