Jessca Nangawe -Dar es salaam
BEKI wa Mtibwa Sugar Issa Rashid maarufu Baba Ubaya amesema timu yao haina udhaifu wowote kiufundi, isipokuwa wanachoamini wamepitia na upepo mbaya ambao utapita na mambo yatakuwa kwenye mstari.
Mtibwa Sugar haijashinda mchezo hata mmoja kati ya minne iliyokwisha shuka dimbani msimu huu.
Ilizindua msimu kwa kuchapwa mabao 3-1na Lipuli, ikalazwa mabao 2-1 na Simba, ikatoka suluhu na JKT Tanzania kabla ya juzi kupokea kichapo cha mabao 3-1 kutoka kwa maafande wa Tanzania Prisons.
Akizungumza mwenendeo huo wa timu yake na hasa baada ya kupoteza mchezo wao dhidi ya Prisons, Baba Ubaya alisema bado timu yao ina makali na uzoefu mkubwa wa kukabiliana na mikiki mikiki ya Ligi Kuu lakini kinachowakuta kwa sasa nyakati mbaya ambazo zitapita muda si mrefu.
“Tuna kikosi kizuri, wengi ni wale wale wachezaji ambao tuna uzoefu wa kucheza Ligi Kuu kwa muda mrefu, nadhani ni upepo mbaya tu, timu iko vizuri kiufundi na hakuna makosa makubwa ambayo tunaweza kusema yameigharimu timu, tunajipanga kwa michezo ya mbele,”alisema beki huyo.
Aliongeza kuwa pamoja na matokeo hayo hawapaswi kukata tama zaidi ya kujipanga upya na kufanyia marekebisho makosa yaliyojitokeza ili kurejea kwenye ligi hiyo kwa kishindo.