24.1 C
Dar es Salaam
Friday, April 19, 2024

Contact us: [email protected]

Azam yakubali ‘mziki’ wa Mbeya City

Ofisa Habari wa klabu ya Azam, Jaffar Iddi
Ofisa Habari wa klabu ya Azam Fc, Jaffar Iddi

Na PENDO FUNDISHA, MBEYA

LICHA ya kupambana na kupata ushindi wa mabao 2-1 kwa taabu katika Uwanja wa Sokoine mkoani Mbeya juzi, klabu ya Azam FC imeapa kwamba haitaweza kukisahau kikosi makini cha Mbeya City walichokutana nacho.

Hii ni mara ya kwanza kwa Azam kuondoka na pointi zote sita katika Uwanja wa Sokoine, huku ikifanikiwa kuvunja mwiko wa kutowafunga maafande wa Tanzania Prisons kwenye uwanja huo.

Akizungumza jijini hapa baada ya mchezo wa juzi, Ofisa Habari wa klabu hiyo, Jaffar Iddi, alisema walipata ushindi kwa tabu ambapo alimpongeza kocha wa Mbeya City, Kinnah Phiri, kwa kazi nzuri aliyofanya kukisuka kikosi chake.

Alisema Azam walijiwekea malengo msimu huu kuhakikisha wanafuta uteja wa kufungwa na kutoa sare mkoani Mbeya, jambo ambalo limefanikiwa kutokana na mikakati waliojiwekea.

Naye kocha mkuu wa timu hiyo, Zeben Hernandez, aliulalamikia Uwanja wa Sokoine akidai kuwa kiwango cha soka kilichoonyeshwa na wachezaji wake si kile alichotegemea kutokana na hali ya uwanja.

“Wachezaji wamecheza kiwango tofauti kabisa kutokana na mazingira waliyokutana nayo, kwani ni tofauti na yale waliyoyazoea kwenye Uwanja wa Chamazi,” alisema Hernandez.

Kwa upande wake, kocha wa Mbeya City, alisema wachezaji wake walitawaliwa na hofu uwanjani, hali iliyosababisha washindwe kupata matokeo mazuri nyumbani na kukubali kipigo dhidi ya Azam.

Kocha huyo raia wa Malawi, alisema hali hiyo iliwapa nafasi wapinzani kutumia uzoefu wao, huku akiwatupia lawama waamuzi kwa madai kuwa hawakutenda haki na walikuwa na kasoro nyingi.

“Hatuwezi kukata tamaa kwa sasa kwani kiwango tulichoonyesha uwanjani ni kikubwa na mashabiki wamefurahia, kazi kubwa iliyobaki ni kujipanga kwa mechi zijazo,” alisema Phiri.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles